Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Chuja:

Habari Mpya

Majambazi wavamia malori ya WFP Uganda

Shirika la UM juu ya Miradi ya Chakula Duniani (WFP) limeripoti kwamba majambazi fulani walishambulia, kwa kuvizia, msafara wa malori ya UM katika jimbo la Karamoja la Uganda kaskazini-mashariki na kumwua dereva, Richard Achuka, 41, tukio ambalo limeilazimisha WFP kusitisha kwa muda operesheni za kuhudumia waathiriwa wa ukame nusu milioni chakula kwenye eneo husika.

Mashirika ya UM yajumuika kukomesha utapiamlo Ethiopia

Shirika la WFP pamoja na Shirika la UM juu ya Mfuko wa Maendeleo kwa Watoto (UNICEF) yamenuia kuisaidia Ethiopia kukabili tatizo la kuviza na kudumaza kwa watoto, tatizo ambalo huchochewa na ukosefu wa lishe bora katika mwili. Mradi huo unatazamiwa kufadhiliwa kutoka msaada wa Kamisheni ya Ulaya (EC) ambayo itajumuika na WFP na UNICEF pamoja na Serekali ya Ethiopia kusaidia wale mama na watoto waliokabiliwa na hali duni kupata huduma za kuboresha lishe na, hatimaye, kuwaepusha vijana na tatizo la kudumaa na kukua na kimo kidogo.

UM kusaidia wanasiasa Sierra Leone kupata welekevu wa vyombo vya habari

Shirika la UM juu ya Miradi ya Maendeleo (UNDP) pamoja na Ofisi ya Kufufua Kadhia za Uchumi na Jamii Sierra Leone (UNIOSIL) yamefanyisha warsha maalumu kwenye mji mkuu wa Freetown, Sierra Leone kuwasaidia wawakilishi wa vyama vya kisiasa kupatiwa uzoefu na welekevu juu ya mbinu za kuwasiliana na umma kwa kueneza ujumbe unaoambatana na itikadi zao za kisiasa, kwa kutumia vyombo vya habari.

Hapa na pale

Jamii ya Kundi la Washauri wa UM juu ya Huduma za Fedha imetangaza taratibu mpya kadha za kuhamasisha jumuia mbalimbali - ikijumuisha serekali, wahudumia maendeleo na pia sekta ya binafsi - kuwasaidia watu masikini, hususan katika mataifa yanayoendelea, kupata fursa ya kushiriki kwenye huduma za fedha, mathalan, uwezo wa kufungua akaunti ya benki, kuchukua mikopo, au kununua bima, huduma ambazo zikitekelezwa zitausaidia umma masikini kuwekeza fedha hizo kuboresha maendeleo katika sekta za uchumi na jamii.

Ripoti ya mfumo wa vikosi vya amani kwa Darfur imekamilishwa

KM Ban Ki-moon amemtumia Raisi wa Baraza la Usalama kwa mwezi Mei, Balozi Zalmay Khalilzad wa Marekani na vile vile Baraza la Usalama la Umoja wa Afrika (AU), ripoti yenye kuelezea, kwa ukamilifu, mfumo wa vikosi vya mseto vya AU na UM vinavyotazamiwa kupelekwa kwenye jimbo la Sudan magharibi la Darfur.

ICTR imeidhinisha hukumu ya kifungo cha maisha dhidi ya M. Muhimana

Korti Ndogo ya Rufaa ya Mahakama ya Kimataifa juu ya Rwanda (ICTR) iliopo Arusha, Tanzania imeidhinisha na kuthibitisha tena ile hukumu ya 2005 ya kifungo cha maisha kwa Mikaeli Muhimana aliyetuhumiwa kuendeleza makosa ya jinai dhidi ya utu katika Rwanda mnamo 1994. Miongoni mwa makosa yaliyomtia hatiani Muhimana ni pamoja na kushtakiwa kushiriki kwenye jinai ya mauaji ya halaiki, vitendo vya kunajisi kihorera wanawake wawili na vile vile kumwua mwanamke mwengine mja mzito.

Vikosi vya MONUC katika DRC vinachunguzwa kuhusu rushwa

Ofisi ya UM ya Kuchunguza Ukiukaji Kanuni za Kazi (OIOS) imeripotiwa kuendeleza ukaguzi wa hali ya juu kuhusu yale madai kwamba vikosi vya ulinzi wa amani vya UM katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo vya Shirika la MONUC, vilihusika na biashara ya magendo ya madini katika kipindi kati ya miaka ya 2005-2006. Tuhuma zilidai vikosi vya MONUC vilinunua madini ya thamani kwa kuwapatia wachuuzi madini hayo silaha, biashara inayodaiwa kuendelezwa kwenye mji wa Mongwalu, Wilaya ya Ituri iliopo Mashariki ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (DRC).