Wakimbizi wa Sudan wengi zaidi nchini CAR, UNHCR yakimbizana na muda kuiwahi mvua
Zaidi ya watu 13,000 kutoka Sudan wamewasili katika Kijiji cha Am Dafock kaskazini mwa Jamhuri ya Afrika ya Kati ili kuepuka madhila ya mgogoro unaoendelea nchini mwao. Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi linasema wengi wa waliowasili ni wanawake na watoto kutoka Nyala mji ulioko kusini magharibi mwa Sudan ambako wanasema walikabiliwa na matatizo kadhaa njiani kuelekea kuvuka mpaka hadi kufika Am Dafock, kama vile vitisho kutoka kwa watu wenye silaha, unyang'anyi wa bidhaa, unyanyasaji wa kimwili na unyanyasaji wa kijinsia.