Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Chuja:

Habari Mpya

Hapa na pale

KM Ban Ki-moon amehuzunishwa na kifo cha Brigedia Jenerali Ahmed Moinuddin, Makamu Kamanda Mkuu wa Vikosi vya Ulinzi Amani vya UM katika Sudan Kusini (UNMIS), ambaye aliuawa Alkhamisi, mnamo tarehe 22 Oktoba, baada ya shambulio liliotukia Islamabad, Pakistan wakati akiwa mapumzikoni. KM alitumia salamu za pole ukoo wa wafiwa, wafanyakazi wa UNMIS na kwa Serikali ya Pakistan, na alitumai watu walioendeleza shambulio, watashikwa haraka na kufikishwa mahakamani.

IAEA imewasilisha maafikiano ya awali kuzingatiwa kuhusu nishati ya nyuklia kwa Iran

Mohamed El Baradei, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la UM juu ya Matumizi ya Amani ya Nishati ya Nyuklia (IAEA) leo Ijumatano aliwaambia waandishi habari wa kimataifa kwamba baada ya siku mbili na nusu ya majadiliano mjini Vienna, taasisi yao imepitisha maafikiano ya awali kuhusu taratibu za kutumiwa kuisaidia Iran kupata nishati itakayotumiwa na kiwanda chao cha kiraia cha kufanyia utafiti wa matibabu.

Ofisa wa UNICEF anasema watoto wamedhurika zaidi na athari za mgogoro sugu wa JAK

Hilde Johnson, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la UM juu ya Mfuko wa Maendeleo kwa Watoto (UNICEF), baada ya kuzuru Jamhuri ya Afrika ya Kati (JAK) ameeleza kwamba matatizo yaliolizonga taifa hilo huathiri pakubwa watoto wadogo, na hali hiihuenda ikaharibika zaidi pindi wahisani wa kimataifa watashindwa kuharakisha misaada inayohitajika kidharura kuhudumia kihali watoto hawa.

Hapa na pale

Asubuhi, Baraza la Usalama lilikutana kusailia hali katika Afrika Magharibi. Haile Menkerios, KM Msaidizi juu ya Masuala ya Kisiasa alipohutubia Baraza la Usalama alizungumzia juu ya ziara yake ya karibuni katika Guinea na maeneo jirani, iliokusudiwa kuandaa utaratibu wa kulisaidia Bodi la Uchunguzi la UM kuendeleza ukaguzi wa vyanzo vya fujo ziliozuka nchini tarehe 28 Septemba mwaka huu. Alisema wadau husika wengi nchini Guinea pamoja na kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo ya Uchumi kwa Mataifa ya Afrika Magharibi (ECOWAS) wote, kwa pamoja, wanaunga mkono rai ya kuanzisha Bodi la Uchunguzi la kimataifa litakaloshughulikia tukio la Septemba. Baada ya mkutano wake na Baraza la Usalama, Menkerios alizungumza na waandishi habari waliopo Makao Makuu, ambao aliwaeleza kuhusu dhamira ya KM ya kuanzisha uchunguzi wa vurugu la Guinea haraka iwezekanavyo, pindi atapatiwa idhini ya kuyafanya hayo na Baraza la Usalama. Menkerios alisema Raisi wa Guinea, Dadis Camara amemuahidi kuwa atashirikiana kikamilifu na tume ya uchunguzi ya UM.

UNHCR inasema wahamiaji wa Angola waliofukuzwa JKK wanahitajia misaada ya dharura ya kuwavua na janga la njaa

Andrej Mahecic, msemaji wa Shirika la UM juu ya Huduma za Wahamiaji (UNHCR) leo asubuhi aliwaarifu waandishi habari Geneva kwamba makumi elfu ya raia wa Angola waliofukuzwa kutoka JKK, ambao sasa wamewekwa kwenye vituo kadha vya makazi ya muda kwenye mji wa Mbanza-Congo, Angola kaskazini, wapo kwenye hali mbaya na wanahitajia misaada ya dharura kunusuru maisha. UNHCR ilipeleka Mbanza-Congo, katika mwisho wa wiki iliopita, ujumbe maalumu wa kutathminia mahitaji ya wahamiaji wa Angola waliofukuzwa kutoka JKK.