Mfanyakazi mmoja wa Kituo cha Kufyeka Mabomu Yaliotegwa Cyprus (MACC), raia wa Msumbiji, aliuawa leo kwenye ajali iliotukia wakati akiendeleza operesheni zake. Kifo hiki ni cha kwanza kutukia. katika miaka mitano ya shughuli hizi kisiwani Cyprus. Mwaathirika wa ajali hiyo anaitwa Femisberto Novele, na alifariki baada ya bomu liliotegwa kuripuka, katika milango ya saa mbili za asubuhi, kwenye uwanja ulioambukizwa vijibomu viliotegwa ardhini, karibu na sehemu ya Geri, iliopi kilomita 10 kusini-mashariki ya mji wa Nicosia. Taye-Brook Zerihoun, Mjumbe Maalumu wa UM kwa Cyprus na mkuu wa Vikosi vya UM Kulinda Amani Cyprus (UNFICYP) alisema alishtushwa na kuhuzunishwa na ajali iliosababisha kifo cha Novele, tukio ambalo, alitilia mkazo, lilikuwa ni msiba kwa UM, unaokumbusha hatari wanayokabiliwa nayo wafanyakazi wa kimataifa wanaohudumi ufyekaji wa mabomu yaliotegwa, ambayo yamenea katika sehemu kadha katika Cyprus. Zerihoun aliwatumia mkono wa pole ukoo wa marehemu Novele, kwa niaba ya timu ya watumishi wa UM waliopo Cyprus. Mradi wa MACC husimamiwa na Shirika la UM juu ya Miradi ya Maendeleo (UNDP) na tangu 2004, wafanyakazi wa Kituo cha MACC walifanikiwa kuondosha na kuangamiza mabomu 14,000 yaliotegwa, na kusafisha maeneo 57 yaliotegwa mabomu, yanayojumuisha kilomita za mraba milioni 6.5 za ardhi.