Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watoto 120 wahitaji haraka matibabu Ghouta:UNICEF

Hasan (kushoto), mvulana mwenye umri wa miaka 10, anakusanya maji kwa ajili ya familia yake katika eneo la Shakoor Mashariki mwa Aleppo. Hasan na marafiki zake wanajaribu kutafuta furaha kwa kucheza pamoja kila siku wanapokusanya maji.Picha: UNICEF

Watoto 120 wahitaji haraka matibabu Ghouta:UNICEF

Takriban watoto 120 wagonjwa mahututi waliokwama kwenye eneo linalozingirwa la mashariki mwa Ghouta nchini Syria wanahitaji kuhamishwa haraka kutoka eneo hilo ili wakatibiwe, limesema shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF. Siraj Kalyango na maelezo zaidi.

(Taarifa ya Siraj Kalyango)

Mwakilishi wa UNICEF nchini Syria Fran Equiza ameiambia UNNews kuwa fursa ya kufikisha misaada ya kibinadamu eneo hilo inaendelea kuwa finyu huku asilimia 12 ya watoto walio na umri wa chini ya miaka mitano wakikabiliwa na utapia mlo uliokithiri.

Wiki za kwanza za mwaka huu zimeshuhudia maelfu kwa maelfu ya watu wakitawanywa upya na mapigano baina ya serikali na majeshi ya upinzani sio tu Mashariki mwa Ghouta na Idlib, lakini pia katika miji mingine ya Hama, Damascus, Aleppo, Hassakeh, Deir EzZour na Raqqa.

Equiza anasema machafuko hayo haswa Ghouta yamekatili maisha ya watoto 30, huku karibu shule zote zimefungwa, na kuna hali mbaya ya upatikanaji wa chakula, au huduma za afya.

Amesema wamebaini kuwa asilimia 12 ya watoto walio chini ya miaka mitano wana utapiamlo na wagonjwa mahtuti wanawekwa tu ndani.