George Clooney ameteuliwa rasmi na UM kuhubiri amani
Mwigizaji Maarufu wa Michezo ya Sinema Marekani, George Clooney, ameteuliwa rasmi wiki hii na KM kuwa Mjumbe Maalumu wa Kuhubiri Amani.
Mwigizaji Maarufu wa Michezo ya Sinema Marekani, George Clooney, ameteuliwa rasmi wiki hii na KM kuwa Mjumbe Maalumu wa Kuhubiri Amani.
KM Ban Ki-moon alipohudhuria Mkutano Mkuu wa Umoja wa Afrika Addis Ababa, Ethiopia alipata fursa ya kukutana kwa muda wa saa na nusu na Raisi Omar al-Bashir wa Sudan, na waliafikiana umuhimu wa kuharakisha kupelekwa vikosi vya ulinzi wa amani vya UNAMID katika Darfur.
KM ameliarifu Baraza la Usalama kuwa ameamua kumteua Victor Da Silva Angelo wa Ureno kuwa Mjumbe Maalumu wa Shirika jipya la Ulinzi wa Amani katika Chad na Afrika ya Kati (JAK) litakalojulikana kama MINURCAT.
Baraza la Usalama, kwa kauli moja, limepitisha azimio la kuongeza muda wa operesheni za amani mipakani Ethiopia na Eritrea kwa miezi sita zaidi, kwa sababu imeripotiwa hali ya wasiwasi bado inaendelea kukithiri kwenye lile eneo la kusitishwa mapigano la TSZ. Mataifa haya mawili vile vile yalinasihiwa kuondosha haraka vikosi vyao ambavyo hivi sasa vimeenezwa kwenye eneo la mgogoro la TSZ.
KM Ban alikuwepo Kigali, Rwanda mwanzo wa wiki na alizuru Makumbusho ya Mauaji Makubwa ya Halaiki. Alisema alihuzunishwa sana na aliyoyashuhudia, na alitoa mchango binafsi wa dola 10,000 kufadhilia mfuko wa Serikali ambao hutumiwa kuwasaidia mamia ya watoto mayatima wa mauaji hayo kupata elimu.
Shirika la UM juu ya Huduma za Wahamiaji (UNHCR) limeripoti kwamba wahamiaji 184 waliorejeshwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo kutokea Tanzania hivi majuzi, wamejumuisha wahamiaji 50,000 – fungu ambalo liliamua kurejeshwa makwao kwa hiyari.
Wiki hii yote UM umeandaa matukio na tafrija kadha wa kadha, katika sehemu mbalimbali za dunia kuwaheshimu na kuwakumbuka waathiriwa wa Maangamizi ya Halaiki, hususan wale wafuasi wa dini ya Kiyahudi.
Ripoti mpya ya KM juu ya hali ya watoto katika maeneo yenye mapigano imebainisha kwamba kuna baadhi ya nchi wanachama ambazo bado zinaendeleza karaha ya kuwalazimisha watoto wadogo kujiunga na makundi ya wanamgambo na kushiriki kwenye mapigano. Mataifa haya, kwa mujibu wa ripoti ya UM, hujumuisha Afghanistan, Burundi, Chad, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Colombia na vile vile Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, Myanmar, Nepal, Philippines, Somalia, Sudan pamoja na Sri Lanka na Uganda.
Shirika la Chakula na Kilimo (FAO) limeripoti kwamba baina ya miaka 1980 hadi 2005 asilimia 20 ya mikoko imeangamizwa duniani kutokana na uharibifu wa mazingira na pia kuzorota kwa uchumi, hasa katika nchi ziliopo Amerika ya Kati na Kaskazini na barani Afrika.