Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Tuondoe vikwazo vya kitamaduni na kimazingira dhidi ya watu wenye ulemavu- Guterres

Mkalimani wa lugha ya ishara katika moja ya vikao maalum kwa watu wenye ulemavu kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa. (Picha:UN/Maktaba)

Tuondoe vikwazo vya kitamaduni na kimazingira dhidi ya watu wenye ulemavu- Guterres

Ikiwa leo ni siku ya kimataifa ya watu wenye ulemavu, Umoja wa Mataifa unapigia chepuo marekebisho yatakayoondoa vikwazo dhidi ya kundi hilo ili malengo ya maendeleo endelevu yanufaishe watu wote.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres katika ujumbe wake amesema msingi mkuu wa kufanikisha hilo ni kuweka mazingira ambamo kwayo hakuna mtu atakayeona ametengwa au ameenguliwa katika kufanikisha malengo hayo.

Mathalani amesema kuwepo kwa miundombinu, teknolojia, huduma na bidhaa ambazo zitanufaisha watu wote wakiwemo watu bilioni moja wenye ulemavu duniani.

image
Nchini Sri Lanka, raia huyu amewezeshwa na sasa anaweza kushiriki katika masuala ya ufundi bila kikwazo chochote. (Picha:ILO)
Bwana Guterres amesema kufanikisha hilo lazima kushirikiana na watu wenye ulemavu ili kubuni, kutengeneza na kutekeleza mbinu bunifu na rahisi za siyo tu kurahisisha Maisha yao bali pia washiriki katika utekelezaji wa ajenda 2030 ya maendeleo endelevu.

Kwa mantiki hiyo Bwana Guterres ametaka nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa kutumia siku ya leo ya watu wenye ulemavu duniani kuondoa vikwazo vya kimazingira na kiutamaduni na hivyo kujenga jamii ambazo zinaweza kukabiliana na mazingira yake na pia kuweka fursa za kuhakikisha hakuna anayeachwa nyuma.