Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Chuja:

Habari Mpya

Upatanishi wa amani unahitajika kuimarisha uhusiano bora kati ya UM na UA, anasihi KM Ban

Baraza la Usalama Ijumatano lilikutana kwenye kikao maalumu, cha hadhi ya juu, kilichofanyika kwenye Makao Makuu mjini New York, kwa madhumuni ya kujadilia namna ya kuongeza ushirikiano halisi na ushikamano wa kuridhisha kati ya UM na taasisi zake, hasa ile taasisi ya Baraza la Usalama, pamoja na Umoja wa Afrika (UA), hususan kwenye juhudi za kuzuia na kutatua kwa amani migogoro iliolivaa bara la Afrika. Kwenye hotuba alioitoa KM Ban Ki-moon katika mkusanyiko wa Baraza la Usalama, alisistiza ya kuwa utaratibu unaochukuliwa na jumuiya ya kimataifa kusuluhisha fujo na mizozo iliopo Afrika, kwa njia za amani, ni lazima ukuzwe na upewe umuhimu wa hadhi ya juu na UM pamoja na Umoja wa Afrika.

Maharamia Darfur wailazimisha WFP kupunguza posho kwa umma muhitaji

Shirika la UM juu ya Miradi ya Chakula Duniani (WFP) limetangaza leo kwamba kuanzia mwezi ujao wa Mei litalazimika kupunguza kwa nusu, ile posho ya chakula inayopeleka kwenye jimbo la uhasama la Darfur, Sudan kwa sababu malori yalioajiriwa na UM yenye kuchukua shehena ya chakula bado yanaendelea kushambuliwa na maharamia. Vitendo hivi tuliarifiwa huzorotisha sana huduma za kufadhilia misaada ya chakula kwa umma muhitaji katika Darfur.

UM unasisitiza, hadhi ya mazungumzo ya upatanishi kwa Sahara ya Magharibi hairidhishi

Ripoti ya karibuni ya KM kuhusu Sahara ya Magharibi imekaribisha, kwa ridhaa kuu, ahadi za makundi husika na mzozo huo, yaani Serikali ya Morocco na kundi la ukombozi wa Sahara Magharibi la Frente POLISARIO, kuendelea kushiriki kwenye majadiliano ya upatanishi. Lakini KM alionya kwamba kasi ya mazungumzo haitoweza kusarifiwa bila ya kwanza \'kukwamua mzoroto uliopo wa kisiasa, kwa moyo wa kuelewana na uhalisia wa kutoka pande zote mbili.\' Ripoti ya KM ilisema hali ya mazungumzo ilivyo sasa hivi haikubaliki kamwe, katika kusukuma mbele juhudi za upatanishi na ni lazima irekibishwe.

EthiopiaEritrea: KM anaonya ulinzi wa UM mipakani ukikomeshwa utaruhusu uhasama kurejea

KM wa UM Ban Ki-moon amewasilisha ripoti maalumu majuzi kuhusu operesheni za Shirika la UM juu ya Ulinzi wa Amani Mipakani Ethiopia/Eritrea (UNMEE), Ripoti imependekeza kwa jumuiya ya kimataifa kuzingatia kidharura changuzi nne muhimu, kusailia kama huduma za amani bado zinahitajika kuendelezwa kwenye eneo la uhasama katika Pembe ya Afrika au zisitishwe, hususan baada ya wenye madaraka Eritrea kuamua kuweka vikwazo kwenye upande wao wa mpaka, hali ambayo ilikwamisha na kozorotisha operesheni za amani za UM.

BU lazingatia uhusiano bora na Umoja wa Afrika

Baraza la Usalama (BU) asubuhi ya leo lilifanyisha kikao maalumu cha hadhi ya juu, kuzingatia taratibu mbadala, zitakazotumiwa kuimarisha uhusiano bora kati ya UM na Umoja wa Afrika, hususan katika huduma za kusawazisha usalama na amani wa kieneo na kimataifa.

Ajali ya ndege katika JKK yaihuzunisha UM

Shirika la UM juu ya Ulinzi wa Amani katika JKK (MONUC) limethibitisha kwamba ndege ya abiria ya kampuni ya ndege inayoitwa Hewa Bora ilianguka na kupasuka hapo Ijumanne, muda tu baada ya kuanza kuruka, katika mji wa kaskazini-mashariki wa Goma katika JKK. Iliripotiwa na Msemaji wa KM kwamba ndege ilikuwa imebeba abiria na wafanyakazi wa ndege 70 ziada.

Wataalamu wasisitiza kilimo cha kisasa chawajibika kuzingatia mahitaji halisi ya umma masikini

Tume ya Kimataifa Maalumu ya Wataalamu 400 waliodhaminiwa bia na Benki Kuu ya Dunia pamoja na mashirika kadha ya UM, imetoa mwito wa dharura uliojumuishwa kwenye ripoti iliopendekeza kufanyike mageuzi makali ya kimsingi, haraka iwezekanavyo, kwenye taratibu zinazotumiwa kuzalisha mazao ya chakula, ili kuhakikisha marekibisho haya mapya yatakidhi zaidi mahitaji ya watu masikini na wale wenye njaa.