Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban awa na mazungumzo na Rais wa bunge la EU

Ban awa na mazungumzo na Rais wa bunge la EU

Kuwa na maafikiano ya dhati kwa ajili ya maendeleo endelevu, SDG baada ya mwaka 2015 na kufikia mkataba wa mabadiliko ya tabianchi mwezi Disemba huko Paris, ni mambo mawili muhimu kwa mwaka huu wa 2015.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon amesema hayo wakati wa mazungumzo yake na Rais wa Bunge la muungano wa Ulaya Martin Schulz, kando mwa kongamano la uchumi la dunia huko Davos, Uswisi.

Ban amesema anategema sana usaidizi wa bunge hilo katika kuunda ajenda ya mabadiliko ya maendeleo endelevu huku akitoa shukrani zake za dhati kwa uongozi wa bunge hilo kwenye masuala ya mabadiliko ya tabianchi.

Wawili hao pia wamejadili hali ya Ukraine pamoja na jitihada za kimataifa za kukabiliana na ugaidi.