Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kilimo cha kaya chapigiwa chepuo: FAO

Kilimo cha kaya chapigiwa chepuo: FAO

Kwa kutambua mchango wa kilimo cha kaya katika kuhakikisha uhakika wa chakula na kutokomeza umaskini duniani, shirika la chakula na kilimo FAO limezindua mfumo mpya wa kidigitali utakaokuwa na taarifa zote muhimu kuhusu kilimo hicho.

FAO imesema mfumo huo utakuwa na taarifa, takwimu na sheria kuhusu sekta hiyo adhimu ambayo ndiyo chanzo cha asilimia 80 ya chakula chote duniani.

Taarifa zitatolewa kwa watafiti, serikali, mashirika ya kimataifa kwa kuzingatia kuwa wakulima wa kaya wanalisha jamii na kuhifadhi dunia.

Francesco Pierri ni mkuu wa kitengo cha utetezi cha FAO kuhusu masuala ya ubia na uwezeshaji anasema taarifa zipo lakini hazipatikani mahali pamoja kwa hiyo...

(Sauti ya Francesco)

“Tunachojaribu kufanya ni kuwa na mahali pamoja pa umma ambapo tunabadilishana taarifa kuhusu kilimo cha kaya ili hatimaye kurahisisha utungaji sera na mijadala,  lakini pia uamuzi wa umma na sera za umma.”

Hatua hii ni matokeo ya mwaka wa kimataifa wa kilimo cha kaya ulioadhimishwa mwaka jana ambao uliangazia mchango na harakati za familia katika kulisha idadi ya watu duniani inayotarajiwa kuongezeka na kufikia Bilioni Tisa mwaka 2050.