Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kuboresha ukusanyaji takwimu kwaonyesha ukubwa halisi wa TB

Wagonjwa wa kifua kikuu kutoka Myanmar wakiishi kwenye vibanda wakati wa matibabu katika Klinik ya Wangpha kwenye mpaka wa Thailand. Picha: IRIN/Sean Kimmons(UN News Centre)

Kuboresha ukusanyaji takwimu kwaonyesha ukubwa halisi wa TB

Jitihada kubwa za hivi karibuni za kuboresha ukusanyaji na utoaji wa taarifa kuhusu kifua kikuu, TB zinaonyesha kuwa kuna visa karibu nusu milioni zaidi vya ugonjwa huo kuliko ilivyokadiriwa awali. Taarifa kamili na Abdullahi Boru.

(Taarifa ya Abdullahi)

Ripoti mpya ya Shirika la Afya Duniani mwaka huu 2014, iliyotolewa leo, inaonyesha kwamba watu milioni 9 waliambukizwa TB mwaka jana. Kati ya hao watu milioni 1.5 walifariki dunia, ikiwa ni pamoja na watu 360 000 ambao walikuwa na Ukimwi.

Hata hivyo, ripoti hiyo ya WHO inasisitiza kuwa viwango vya vifo kutokana na TB vinazidi kupungua, ikieleza kuwa tangu mwaka wa 1990 vifo vimeshuka kwa asilimia 45, huku idadai ya watu wanaoambukizwa ugonjwa huo ikipungua kwa wastani asilimia 1.5 kila mwaka.

Aidha, WHO inasema maisha ya watu wanaokadiriwa kuwa milioni 37 yameokolewa kupitia uchunguzi wenye ufanisi na matibabu tangu mwaka 2000. Dr. Mario Raviglione ni Mkurugenzi wa Mpango wa Kimataifa wa TB katika WHO.

“Kuwa na taarifa bora zaidi kunatuleta karibu zaidi  na ufahamu wa mzigo halisi wa kifua Kikuu”