Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNICEF yapongeza stahamala kwa ajili ya watoto

UNICEF yapongeza stahamala kwa ajili ya watoto

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF limekaribisha taarifa ya pamoja iliyotolewa na madhehebu ya kidini nchini Myanmar kwa ajili ya watoto.

Kupitia tamko la pamoja, viongozi wa madhehebu ya kibudha , kikristu, kihindu na kiislamu, wametoa wito wa kuheshimu uhuru wa kuabudu na kuvumiliana kama sharti muhimu kwa kila mtoto kukua na kustawi ili kufika uwezo wake kamili , bila kujali dini au wazazi wao.

Viongozi hao wamesema haki za watoto ni lazima ziwekwe katika mstari wa mbele wakati wa uchaguzi mwaka 2015, wakati huu ambapo majaribio ya kutumia mgawanyiko wa kidini kama mtaji wa kisiasa yameanza kushamiri.

Wamekumbusha wanasiasa na wananchi kuwa watoto ni karibu theluthi moja ya wakazi wote Myanmar na kwa hiyo, wanachoweza kuwafanyia sasa, kitakuwa na manufaa katika maisha yao ya baadaye.

Mwakilishi wa UNICEF nchini Myanmar, Bertrand Mainvel, amesema viongozi wa kidini wana jukumu kubwa katika kutetea haki za watoto na kupata imani ya waumini wao.