Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mamlaka ya uhamiaji Libya msikiuke haki za binadamu: Zeid

Idadi ya wahamiaji waliozuiliwa nchini Limbya katika hali mbaya yaongezeka. Picha: OHCHR

Mamlaka ya uhamiaji Libya msikiuke haki za binadamu: Zeid

Kamishna Mkuu wa haki za binadamu kwenye Umoja wa Mataifa Zeid Ra'ad Al Hussein leo ameonyesha wasiwasi wake kutokana na ongezeko kubwa la wahamiaji walio  vifungoni katika     vituo mbalimbali  nchini Libya, akisema sera ya Umoja wa Ulaya ya kusaidia ulinzi wa pwani  ya Libya ili kuzuia wahamiaji kuingia barani  humo  inakiuka haki za binadamu.

Bwana Zeid amesema mateso ya wahamiaji waliofungwa Libya ni ukiukwaji wa haki za kibinadamu na kinyume cha ustaarabu kwa mtu yeyote, huku  akiongeza kuwa  njia mbadala  za kuwekwa kizuizini zinaweza kuokoa maisha ya wahamiaji na usalama wao kimwili, pia  kuwalinda kutokana na mateka toka kwa wanamgambo.

Aidha Bwana Zeid amesema kuwa jumuiya ya kimataifa  haitaendelea kufumbia  macho hali  ya wahamiaji huko Libya, huku  akitaka kuundwa kwa hatua za kisheria  ili kuboresha sera za  uhamiaji ili kuhakikisha ulinzi wa haki za binadamu unatekelezwa Libya.

Kulingana na takwimu ya  idara ya kupambana na uhamiaji haramu Libya (DCIM) watu 19,900 wako chini ya  udhibiti  wa idara hiyo  tangu  mapema mwezi huu ikiwa ni idadi kubwa ikilingannishwa na watu 7,000 Septemba wakati wa migogoro ya huko Sabratha.

Ofisi ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa inashauri mamlaka ya Libya kuchukua hatua thabiti ili kuondokana na ukiukwaji wa haki za binadamu katika vituo vya uthibiti wa wahamiaji nchini humo.