Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kuwekeza katika elimu ndio jawabu kwa dunia na mustakabali bora- Guterres

Kuwekeza katika elimu ndio jawabu kwa dunia na mustakabali bora- Guterres

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António  Guterres amesema dunia inakabiliwa na janga la kielimu na bila juhudi hivi sasa, zaidi ya vijana milioni 825 kati ya vijana bilioni 1.6 wataachwa nyuma ifikapo ukomo wa malengo ya maendeleo endelevu SDGs, mwaka 2030.

Akizungumza kwenye kikao kuhusu ufadhili kwa ajili ya elimu kandoni mwa mjadala wa wazi wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, Bwana Guterres amesema yeye binafsi alishuhudia jinsi hatua za kuweka elimu kama haki ya msingi zilivyochochea maendeleo uendelevu na amani.

Kwa hiyo ametaja maeneo manne ambayo yanahitaji kuimarishwa ambayo mosi ni ufadhili ili kuwekeza katika elimu kwa ajili ya kuimarsiha maendeleo kiuchumi, pili kulenga wasichana ambao wanakabiliwa na vikwazo ikiwemo ukatili wa kijnsia na tamaduni potofu, tatu kuhakikisha elimu ya muda mrefu kwa ajili ya stadi za kazi siku zijazo na nne kulenga watoto na vijana walioathirika na mizozo ambao wanakosa fursa kwa ajili ya mazingira waliyomo.

Hivyo amesema

image
Katibu Mkuu wa Umoja huo António Guterres akizungumza kwenye kikao kuhusu ufadhili kwa ajili ya elimu kandoni mwa mjadala wa wazi wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa. Picha: UM/Rick Bajornas
(Sauti ya Guterres)

“Wengi katika chumba hiki tuna uwezo, tunazo rasilimali na huduma kuhakikisha familia zetu wanapata elimu bora. Hebu tudhamirie kama familia ya mataifa kuhakikisha elimu bora kwa watoto wote ulimwenguni. Kuwekeza katika elimu ndio uwekezaji mzuri kwa ajili ya dunia bora na mustakabali bora.”

Naye Malala Yousfzai, mwanaharakati na mtetezi wa elimu ya mtoto wa kike, amesema wasichana milioni 130 hawaendi shule na wanakabiliana na changamoto za umaskini, mizozo na ndoa za utotoni lakini..

(Sauti ya Malala)

image
Malala Yousfzai(kulia), mwanaharakati na mtetezi wa elimu ya mtoto wa kike akizungumza kwenye kikao kuhusu ufadhili kwa ajili ya elimu kandoni mwa mjadala wa wazi wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa. Picha: UM/Rick Bajornas
“SDGs ilikuwa ahadi kwamba tungepigania mengi na wasichana hawa, lakini kufikia sasa, tunawaangusha na zaidi tunajiangusha, wakati wasichana hawaendi shule wanapoteza fursa ya kufuata ndoto zao na dunia inakopoteza uwezo wao.” 

Kwa upande wake Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa zamani wa Tanzania na mjumbe wa kamisheni ya kimataifa kuhusu ufadhili wa fursa za elimu duniani amesema kwamba suala la ufadhili bado ni changamoto kwani kumeshuhudiwa kupungua kwa ufadhili kutoka asilimia 13 hadi 10 katika muongo mmoja.

Hata hivyo

(Sauti ya Kikwete)

“Ni lazima nchi zitenge fedha zaidi kwa ajili ya mahitaji ya elimu na jumuiya ya kimataifa inapaswa kusaidia nchi kwani pekee yake haziwezi. Jumuiya ya kimataifa iingilie kati kupiga jeki juhudi za nchi hizi.”