Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ukatili wa kingono hauna nafasi kwenye UM na dunia yetu:Guterres

Ukatili wa kingono hauna nafasi kwenye UM na dunia yetu:Guterres

Unyanyasaji na ukatili wa kingono hauna nafasi katika dunia yetu,  ni zahma ya kimataifa na ni lazima utokomezwe.

Kwa msisitizo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ametoa wito huo mbele ya hadhira ya kimataifa hi leo wakati wa mkutano wa ngazi ya juu kuhusu unyanyasaji na ukatili wa kingono kwenye Umoja wa Mataifa ikiwemo operesheni zake za ulinzi wa amani akiwaahidi kwamba

(GUTERRES SEA CUT 1)

“Tuko hapa kuchukua hatua za haraka na madhubuti zinazohitajika kukata mizizi ya unyanyasaji na ukatili wa kingono mara moja na daima kwenye Umoja wa Mataifa, na tuko hapa kwa ajili ya mshikamano kujikita mahsusi na tabia za watu binafsi wanaotumia mamlaka yao kuwadhulumu wale wanaoutegemea Umoja wa Mataifa kwa ulinzi.”

Ameongeza kuwa Umoja wa Mataifa hautoruhusu vitendo hivyo potofu vya wachache kupaka matope kazi nzuri ya maelfu ya wanawake na wanaume wanaozingatia maadili ya katiba ya Umoja wa Mataifa. Hata hivyo amesema

(GUTERRES CUT 2)

“Hakuna nchi , hali na wala familia iliyo na kinga dhidi ya unyanyasaji na ukatili wa kingono. Lakini umoja wa Mataifa una wajibu maalumu wa kuweka viwango vya kimataifa katika kuzuia, kuchukua hatua na kuukomesha uhalifu huu na kushughulikia athari zake, kiutu na kwa haki.”

image
Michezo ya kuigiza, muziki na ngoma za zanaa za kuhamasisha #zerotolerrance. Picha: MONUSCO_Conduct in field missions
Amesema  inauma sana kusema kuwa tabia hiyo mbaya imetapakaa kwenye mfumo mzima wa Umoja wa mataifa kwa askari na wafanyakazi raia na katika mazingira mbalimbali ikiwemo kwenye migogoro ya kibinadamu hadi operesheni za ulinzi wa amani na hata kwenye makambi ya wakimbizi ambako watu hawajiwezi na hakuna usalama. Ametoa wito kwa nchi wanachama kushikama na Umoja wa Mataifa katika kukata mzizi huu wa fitna.

Naye Rais wa baraza kuu kikao cha 72 Miloslav Lajcak akizungumza kwenye mkutano huo amesema , maneno matupu hayavunji mfupa

(LAJCAK CUT)

“Ingawa uhalifu tunaouzungumzia leo ni mkubwa sana idadi ya walioutekeleza sio kubwa, nataka kusisitiza kwamba unyanyasaji na ukatili wa kingono unaofanywa na wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa ni lazima ulaaniwe vikali, lakini ni lazima pia tukumbuke kwamba kulaani pekee hakutoshi, tunachohitaji sasa ni hatua.”