Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watoto washirikishwe katika kupambana na mabadiliko ya tabianchi- UNICEF

Picha@UNICEF(UN News Centre)

Watoto washirikishwe katika kupambana na mabadiliko ya tabianchi- UNICEF

Watoto wanaathiriwa zaidi na mabadiliko ya tabianchi na ongezeko la gesi chafuzi hewani, kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa jana na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto, UNICEF.

Mkurugenzi Mtendaji wa UNICEF, Anthony Lake, amesema, asilimia 99 ya vifo vitokanavyo na mabadiliko ya tabianchi vimetokea katika nchi zinazoendelea, na wengi wa waathirika ni watoto.

Vifo hivyo vinasababishwa na majanga ya hali ya hewa kama vile mafuriko, milipuko ya magonjwa, ukosefu wa usalama wa chakula au ukosefu wa upatikanaji wa maji na usafi.

Ripoti ya UNICEF inasisitiza umuhimu wa kushirikisha watoto kwenye mazungumzo kuhusu tabianchi, si tu kwa sababu ni haki yao kama wahanga wa mabadiliko ya tabianchi, bali pia kwa sababu watarithi ulimwengu na matatizo yake, na wao ndio watakuwa na jukumu kubwa la kubadilisha jinsi ya kutumia rasilimali.