Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ingawa umasikini umepungua bado kuna kibarua kikubwa:Ban

Ingawa umasikini umepungua bado kuna kibarua kikubwa:Ban

Maadhimisho ya siku ya kimataifa ya kutokomeza umasikini mwaka huu yanafanyika wakati jumuiya ya kimataifa ikikabiliana na malengo makubwa mawili, kwanza juhudi za kufikia malengo ya amendeleo ya milenia na kuunda malengo mengine yatakayoiongoza dunia baada ya mwaka 2015. Hayo yamesemwa na Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban ki-moon. Taarifa kamili na Assumpta Massoi.

(TAARIFA YA ASSUMPTA MASSOI)

Akitoa ujumbe maalumu wa siku ya kutokomeza umasikini ambayo huadhimishwa kila mwaka Oktoba 17, Ban amesema ajenda ya baada ya 2015 lazima iweke suala la kutokomeza umasikini kama kitovu na maendeleo endelevukamakiini. Kwani amesema njia pekee ya kutokomeza umasikini ni kwa kuiongoza dunia katika maendeleo endelevu.

(SAUTI YA BAN)

Tuna kazi kubwa mbele yetu, wakati umasikini umepungua , mchakato hauko sawia. Mafanikio yetu ya kupunguza uamsikini kwa nusu yasipofushe ukweli kwamba zaidi ya watu bilioni 1.2 bado wanaishi kwenye umasikini uliokithiri duniani kote, wengi sana hususani wanawake na wasichana, wanaendelea kunyimwa huduma bora za afya na usafi, elimu bora na makazi yanayostahili, huku vijana wengi wakikosa ajira na ujuzi unaohitajika kwenye soko la sasa”

Ban ameongeza kuwa ili kuwa na mtakhbali tunaoutaka kwa wote ni lazima kusikiliza na kutekeleza wito unaotolewa na wasiojiweza. Nao wananchi wa maziwa makuu wana maoni gain kuhusu siku hii? Mwandishi wetu wa Bujumbura Ramadhani KIBUGA amekwenda  katika mtaa  duni  wa Buterere,   nje kidogo ya jiji la Bujumbura na kuzungumza na baadhi ya wakaazi wa eneo hilo wanaofanya shughuli mbalimbali.