Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watu saba wamethibitishwa kuwa na Ebola na mmoja kufariki dunia Uganda:WHO 

Mhudumu wa afya akipima joto la mwananchi kwenye eneo la mpakani mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC na Uganda. Wahudumu wa afya kwenye kituo hiki wamekuwa wakichukua vipimo kubaini iwapo wananchi wana Ebola au la. (12 Feb 2019)
UNICEF/Jimmy Adriko
Mhudumu wa afya akipima joto la mwananchi kwenye eneo la mpakani mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC na Uganda. Wahudumu wa afya kwenye kituo hiki wamekuwa wakichukua vipimo kubaini iwapo wananchi wana Ebola au la. (12 Feb 2019)

Watu saba wamethibitishwa kuwa na Ebola na mmoja kufariki dunia Uganda:WHO 

Afya

Shirika la afya la Umoja wa Mataifa duniani WHO limesema linaongeza juhudi zake za kudhibiti kusambaa kwa mlipuko mpya wa Ebola nchini Uganda ambako hadi sasa wagonjwa saba wa Ebola aina ya sudan wamethibitishwa  kikiwemo kifo cha mtu mmoja.  

Tangazo hilo limekuja siku mbili baada ya WHO kuthibitisha kisa cha kwanza baada ya shuku ya vifo sita kwenye wilaya ya Mubende mapema mwezi huu. 

Watu 43 waliowasiliana kwa karibu wa marehemu hao wameshabainishwa na 10 wanaaminika kuambukizwa virusi hivyo vya Ebola na hivi sasa wanapatiwa matibabu kwenye hospitali ya rufaa ya mkoa iliyopo Mubende na kufanya hii kuwa mara ya kwanza Uganda kubaini virusi vya Ebola aina ya Sudan tangu mwaka 2012. 

Mubende ipo katika mkoa wa Kati nchini Uganda karibu saa mbili kwa usafiri wa gari kutoka mji mkuu Kampala katika barabara yenye pilika nyingi ya kuelekea nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC. 

Katika eneo hilo kuna mgodi wa dhahabu ambao unavutia watu kutoka sehemu mbalimbali za Uganda pamoja nan chi nyingine. 

WHO imeeleza kwamba sababu ya mwenendo wa watu kusafiri sana katika eneo kuna hatari kubwa ya virusi kusambaa zaidi. 

Chanjo ya Ebola yaanza nchini Guinea ili kuzuia mlipuko mpya.
WHO
Chanjo ya Ebola yaanza nchini Guinea ili kuzuia mlipuko mpya.

 Hatua zinazochukuliwa na WHO 

Hatua zinazochukuliwa na shirika la WHO dhidi ya mlipuko huo zinahusisha kusambaza vifaa vya matibabu, kutoa vifaa na kupeleka wafanyikazi kusaidia mamlaka ya Uganda katika kuzuia kusambaa kwa virusi hivyo. 

Timu ya kiufundi imetumwa katika wilaya ya Mubende kusaidia ufuatiliaji, kuzuia na kudhibiti maambukizi, na pia usimamizi wa wagonjwa waliothibitishwa. Ufuatiliaji unafanywa kwa kasi katika wilaya jirani, na wahudumu wa ndani  wa afya wako mstari wa mbele, ili kuimarisha juhudi za kupambana na Ebola. Wataalam watano wa kimataifa pia wanatumwa, na wengine zaidi wako tayari Kwenda ikiwa wanahitajika. 

"Tunachukua hatua za haraka na madhubuti kuhakikisha udhibiti wa mlipuko huu. Utayari wa dharura wa nyumbani wa Afrika unaonekana kuwa muhimu zaidi katika kukabiliana na milipuko kama vile Ebola" amesema Dkt. Abdou Salam Gueye, mkurugenzi wa dharura wa kanda katika ofisi ya WHO Kanda ya Afrika. 

Maendeleo ya chanjo 

WHO imesema Ebola inaweza kuwa mbaya, lakini utambuzi wa mapema wa dalili na wagonjwa huongeza sana fursa za watu kuishi. 

Hakuna chanjo yoyote miongoni mwa chanjo zilizopo  sasa za Ebola yenye ufanisi dhidi ya aina ya Sudan iliyotgundulika nchini Uganda, lakini angalau kuna chanjo sita ambazo ziko katika hatua tofauti za maendeleo ya kutengenezwa. 

Timu ya mpango wa utafiti na maendeleo ya WHO inawasiliana na watengenezaji wote wa chanjo na inaongoza juhudi shirikishi zinayohusisha wataalam wa kimataifa ili kubaini ni chanjo gani inaweza kufaa kwa tathmini ya ziada wakati wa mlipuko huu, ikiwa wagonjwa zaidi watathibitishwa.