Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Umoja wa Mataifa bado imejizatiti kusaidia Libya

Umoja wa Mataifa bado imejizatiti kusaidia Libya

Umoja wa Mataifa umesema shambulio la gruneti dhidi ya msafara wa watendaji wake nchini Libya jana Jumatano halitateteresha azma ya kusaidia kusaka suluhu ya amani ya kudumu nchini humo.

Shambulio hilo lilitokea wakati msafara wa magari ukiwa na watu 14 ambapo gruneti lililenga moja ya magari yao na kusababisha majeraha kwa dereva mmoja.

Akihojiwa na Idhaa ya Umoja wa Mataifa, Naibu Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Libya Maria do Valle Ribeiro amesema suala la usaidizi halitatatereka hivyo..

(Sauti ya Maria)

“Umoja wa Mataifa unasalia na azma yake thabiti ya kusaidia wananchi wa Libya katika mchakato wa kisiasa na pia kuwapatia misaada ya kibinadamu na kusaidia, kurejesha utulivu, kujikwamua na kusaidia kwa ujumla Libya iondoke katika hali ya sasa ili waweze kunufaika na matunda ya nchi yao.”

Bi. Ribeiro ambaye pia ni Naibu Mkuu wa ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Libya, UNSMIL amesema hadi sasa hawajathibitisha kama ni shambulio lililokuwa limelenga mahsusi msafara wa Umoja wa Mataifa.