Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UM wazitaka pande zote Malakal kusitisha uhasama mara moja-UNMISS

UM wazitaka pande zote Malakal kusitisha uhasama mara moja-UNMISS

Mpango wa Umoja wa mataifa nchini Sudan Kusini UNMISS umesalia na hofu baada ya kuzuka mapigano baina ya SPLA na SPLA ya upinzani kwenye mji wa Malakal na viunga vyake ikiwemo uvurumishaji wa makombora ulioripotiwa katika siku chache zilizopita.

UNMISS imearifu kwamba Jumapili hali katika mji wa Malakal imekuwa na wasiwasi, mji ukiwa umetelekezwa kwa kiasi kikubwa ingawa mpango huo umeendelea kushika doria katika mji huo.

Mpango huo wa Umoja wa Mataifa umerejea wito wake wa kuzitaka pande zote katika mzozo kusitisha uhasama mara moja na kutekeleza makubaliano ya amani. UNMISS imesema itaendelea kulinda raia wa Sudan Kusini walio hatarini huku ukizisistiza pande zote kunyamazisha mtutu wa kubundi na kuruhusu wafanyakazi wa misaada ya kibinadamu kuingia katika maeneo yaliyoathirika.