Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

FAO inasaka ufadhili wa haraka kusaidia watu 385,000 Nigeria

FAO inasaka ufadhili wa haraka kusaidia watu 385,000 Nigeria

Dola milioni 10 zinahitajika ili kutoa msaada wa haraka kwa wakimbizi wa ndani na familia zinazowahifadhi nchini Nigeria. Brian Lehander na ripoti kamili.

(Taarifa ya Brian)

Kwa mujibu wa taarifa ya shirika la chakula na kilimo duniani, FAO iliyotolewa leo, watu Laki Tatu na Elfu Themanini na Watano wanahitaji msaada wa pembejeo za kilimo na kujikimu kimaisha katika eneo la Kaskazini Mashariki mwa Nigeria ambako kuna matatizo ya uhakika wa chakula kutokana na ukosefu wa usalama.

Shirika hilo linasema kuanza shughuli za kilimo hivi sasa ni muhimu sana ili kuhakikisha kwamba watu wanazalisha chakula cha kutosha kwa mahitaji yao, ikiwa ni pamoja na wakimbizi wa ndani waliotawanywa na machafuko pamoja na jamii ambazo zinawahifadhi.

Zaidi ya watu milioni tatu wameathirika na matatizo ya uhakika wa chakula kwenye majimbo ya Borno, Yobe na Adamawa.