Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban azungumza na Kiir; ataka vikosi vya usalama vizingatie sheria za kimataifa za kibinadamu

Ban azungumza na Kiir; ataka vikosi vya usalama vizingatie sheria za kimataifa za kibinadamu

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon amekuwa na mazungumzo kwa njia ya simu na Rais Salva Kiir wa Sudan Kusini kuhusu mapigano yaliyoanza mwishoni mwa wiki nchini humo na kusababisha sinforahamu ikiwemo raia kusaka hifadhi kwenye ofisi za Umoja huo mjiniJuba.

Bwana Ban ameeleza wasiwasi wake juu ya ripoti ya mapigano kati ya wanajeshi SPLA na ya kwamba baadhi ya jamii ni walengwa wa mapigano hayo. Amesema ni matumaini yake kuwa hali ya usalama itarejea Juba haraka iwezekanavyo na raia wataweza kurejea makwao. Ametaka pande zote kumaliza chuki baina yaona serikali ihakikishe kuwa katika udhibiti wa hali hiyo raia wanalindwa bila kujali makabila yao.

Katibu Mkuu ameitaka serikali ya Sudan Kusini kufanya mashauriano na wapinzani wao ili kumaliza tofauti zao kwa amani na kwamba Umoja wa Mataifa uko tayari kusaidia serikali hiyo wakati huu mgumu.

Halikadhalika amemsihi Rais Kiir ahakikishe kuwa vikosi vya usalama vinaendesha operesheni zao kwa kuzingatia sheria za kibinadamu za kimataifa na kwamba ni matumaini yake kuwa Rais atadhihirisha uongozi wakati huu muhimu ikiwemo kurejesha nidhamu baina ya askari wa SPLA wanaopigana bainayao.