Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Siku ya kupinga rushwa, Ban atuma ujumbe, UNDP yaratibu mjadala

Siku ya kupinga rushwa, Ban atuma ujumbe, UNDP yaratibu mjadala

Leo ni siku ya kimataifa ya kupinga rushwa duniani ambapo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon ametaka nchi duniani kutekeleza mkataba wa kimataifa wa kupinga vita rushwa uliopitishwa miaka 10 iliyopita kwani ufisadi au rushwa ni kikwazo kikubwa cha kutimiza malengo ya maendeleo ya milenia na hivyo unahitaji kuvaliwa njuga katika kupanga na kutekeleza ajenda za baada ya mwaka 2015. Taarifa zaidi na Assumpta Massoi

(Taarifa ya Assumpta)

Ban amesema rushwa inazototesha ukuaji wa uchumi kwa kuongeza gharama na kuwa kizingiti katika udhibiti wa mazingira na mali asili.

Ameongeza kuwa rushwa inakwenda kinyume na misingi ya haki za binadamu, inachagiza umasikini na kuongeza pengo la kutokuwepo na usawa katika Nyanja mbalimbali zikiwemo elimu, huduma za afya na huduma zingine na michezo.

Mjini New York, shirika la mpango wa maendeleo la Umoja wa Mataifa, UNDP limefanya mjadala kuhusu rushwa na madhara yake katika malengo ya milenia na hata ajenda ya maendeleo endelevu iwapo haitatokomezwa. Helen Clark, Mkuu wa UNDP akinukuu Benki ya dunia....

(Helen Clark)

Benki ya dunia inakadiria kuwa rushwa inaweza kugharimu nchi hadi asilimia 17 ya pato lake na ndani. Rushwa inazuia uwekezaji wa umma na hata ule wa kibinafsi kuelekezwa pale inapohitajika zaidi, inaongeza gharama na hata kuharibu vipaumbele vya umma.”