Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Awamu ya kwanza ya kuthibitisha silaha za kemikali nchini Syria yakamilika:

Awamu ya kwanza ya kuthibitisha silaha za kemikali nchini Syria yakamilika:

Ripoti kutoka The Hague, Uholanzi zinasema kuwa wataalamu katika timu ya pamoja ya Umoja wa Mataifa na shirika la kimataifa la kupinga matumizi ya silaha za kemikali, OPCW wamehitimisha awamu ya kwanza ya kukagua na kuthibitisha silaha za kemikali nchini Syria.  Inaelezwa kuwa hadi Jumapili tarehe 27 mwezi huu, wataalamu walishakagua na kutambua maeneo 21 kati ya 23. Maeneo hayo mawili hayakuweza kukaguliwa kutokana na sababu za kiusalama na jitihada zinaendelea ili  kuhakikisha mazingira ni salama kwa wakaguzi kuweza kuyafikia. Ripoti zinasema kuwa Syria ilikabidhi taarifa rasmi kuhusu mpango wake wa silaha za kemikali siku tatu kabla ya tarehe ya mwisho ambayo ni jana, ambapo taarifa hiyo ilihusisha pia mikakati ya kutokomeza silaha hizo ili uweze kuzingatiwa na baraza tendaji la OPCW. Ujumbe wa pamoja wa UM na OPCW uliundwa hivi karibuni ili kufanikisha kazi ya kuteketeza mpango wa silaha za kemikali wa Syria kwa muda muafaka na kwa usalama zaidi.