Jopo la UM lasubiri kibali kutoka serikali ya Syria
Jopo la Umoja wa Mataifa lililoundwa kuchunguza madai ya matumizi ya silaha za kemikali huko Syria litaenda nchini humo mapema iwezekanavyo pindi serikali itakaporidhia mpango kazi wake. Kauli hii ya hivi punde ni taarifa kutoka kwa msemaji wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kwenda kwa waandishi wa habari ambapo amesema mwishoni mwa wiki iliyopita, mkuu wa jopo hilo Profesa Ake Sellström kutoka Sweden alikamilisha maandalizi yanayotakiwa kwa ajili ya ziara hiyo nchini Syria. Kinachosubiriwa hivi sasa kwa mujibu wa taarifa hiyo ni kibali cha kuridhia kutoka serikali ya Syria. Wakati huo huo, Mkuu wa masuala ya kutokomeza silaha wa Umoja wa Mataifa Angela Kane ameendelea na mashauriano yake na serikali ya Syria kwa minajili ya kufikia makubaliano haraka iwezekanavyo juu ya mpango kazi na hatimaye jopo la Umoja wa Mataifa liweze kufanya kazi yake kwa usahihi, usalama na lijitosheleze.