Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ukatili kwa wanawake wahusiana na uhakika wa chakula: Mashirika UM

Ukatili kwa wanawake wahusiana na uhakika wa chakula: Mashirika UM

Wakati leo ni siku ya wanawake duniani, mashirika ya Umoja wa Mataifa yanayohusika na chakula kwa pamoja yametoa taarifa yakiweka bayana uhusiano kati ya ukatili wanaofanyiwa wanawake na uhakika wa chakula.

Mashirika hayo lile la chakula na kilimo, FAO, maendeleo ya kilimo na chakula IFAD, mpango wa chakula duniani, WFP pamoja na shirika la kimataifa linalosimamia sheria kwa maendeleo, IDLO,  yamesema licha ya kwamba wanawake wana mchango mkubwa katika kuzalisha chakula na kupatia mlo familia zao, bado kuna jitihada ndogo za kuhusisha ukatili wa kijinsia na uhakika wa chakula.

Mathalani yamesema ubaguzi wa kijinsia unachochea utapiamlo miongoni mwa wanawake  ambapo yamesema mara nyingi ubaguzi vijijini huibua upendeleo katika mgao wa vyakula ndani ya familia ambapo wanawake na watoto wa kike hupata chakula kidogo na lishe duni.

Halikadhalika yamesema wakati wa msimu wa njaa, familia maskini huweza kuoza watoto wao wa kike wenye umri mdogo kwa lengo la kupunguza idadi ya watu wanaopatiwa mlo ndani ya familia.

Mashirika hayo yamesema iwapo watu wote wataungana kuongeza uhakika wa chakula miongoni mwa wanawake basi watakuwa wanaimarisha fikra na miili ya jamii nzima.