Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Uganda yapitisha amri ya kutotembea usiku kudhibiti COVID-19

Watu wengi wamepoteza ajira kufuatia hatua zilizochukuliwa kuzuia kusambaa kwa COVID-19.
UN News/ John Kibego
Watu wengi wamepoteza ajira kufuatia hatua zilizochukuliwa kuzuia kusambaa kwa COVID-19.

Uganda yapitisha amri ya kutotembea usiku kudhibiti COVID-19

Sheria na Kuzuia Uhalifu

Uganda imefuata nyayo ya baadhi ya nchi duniani ya kupitisha amri ya kutotembea usiku kama mojawapo ya njia za kuzuia kuenea kwa ugonjwa wa virusi vya Corona, au COVID-19, sanjari na kufunga mipaka yake na kupiga marufuku usafiri wa magari binafsi.

Rais Yoweri Kaguta Museveni ametangaza maagizo mapya kabisa kwa madhumuni ya kuzuia kusambaa zaidi kwa virusi hivyo nchini Uganda.

Amri kubwa zaidi ni zile sheria ya kutotembea usiku isipokuwa magari ya mzigo, kubana mikutano ya watu zaidi ya watano kutoka 10 waliokuwa wamekubaliwa katika maagizo ya kwanza, kuagiza wahudumu wa umma kusalia majumbani ila wale wanaohusika na vita dhidi ya COVDI-19 wakiwemo wauguzi na waganga wa mifugo,  askari na wafanyakazi wa makampuni yanayotoa huduma za maji na umeme.

 Kulingana na Raisi Museveni, maagizo 16 ya ziada yametolewa kutokana na wananchi kutotii maagizo ya kwanza kama ilivyotarajiwa kiasi kwamba magari binafsi yaligeuzwa kuwa ya abiria kisiri na kusawazisha malengo ya kubana usafiri wa umma,“Magari binafsi yalikuwa yamegeuzwa kuwa vyombo vipya vya usafiri wa umma bila leseni huku wakiongeza uwezekano wa maambukizo. Marufuku dhidi ya usafiri binafsi uliokuwa umegeuzwa kuwa wa abiria inaanza kutekelezwa saa nne za usiku wa leo. Kuanzia saa moja ya usiku wa tarehe 31 Machi hamna kutembea usiku kote nchini na maduka yote yasio ya chakula ni lazima yafungwe”

Magari yote ya serikali yataegeshwa kwenye  makao makuu ya serikali za mitaa na madereva wao tayari kuitikia dharura yoyote kuhusu COVID-19, kwa usimamizi wa kamati mahsusi za kupambana na virusi hivyo.

Masoko ya chakula yataendelea na kazi endapo tu mamlaka zao za usimamizi zitahakikisha kwamba wachuuzi hawarejei majumbani hadi mwisho wa siku 14 za maagizo haya mapya na kutii maagizo yote wizara ya afya kuhusiana na COVID-19.

Amewashauri kujenga mahema nje ya masoko husika kuliko kurejea majumbani kila jioni kinachohatarisha familia na jamii zao. Kutokwenda nyumbani kila siku pia kunahusu wafanyakazi wa viwandani na makampuni ya ujenzi wanaotaka kuendelea na akzi wakati huu wa tahadhari ya COVID-19.