Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

COVID-19: Uganda yapiga marufuku wakimbizi kuingia nchini humo

Uchunguzi wa virusi vya Ebola kwenye mpaka kati ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo , DRC na Uganda
WHO/Matt Taylor
Uchunguzi wa virusi vya Ebola kwenye mpaka kati ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo , DRC na Uganda

COVID-19: Uganda yapiga marufuku wakimbizi kuingia nchini humo

Wahamiaji na Wakimbizi

Serikali ya Uganda imesema kutokana na kuenea kwa ugonjwa wa virusi vya Corona, COVID-19,  na idadi ya wagonjwa kufikia 14, wakimbizi hivi sasa hawataingia nchini humo huku ikizuia hata huduma za kudhibiti kuenea kwa virusi hivyo zilizokuwa zikitolewa na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR kwenye vituo vya mapokezi ya wakimbizi.

Taarifa iliotolewa leo kuhusu msimamo wa serikali kwa wakimbizi wanaopitia migogoro isiojali mlipuko wa COVID-19 duniani, Musa Ecweru naibu waziri wa wakimbizi na kushughulikia majanga ametangaza rasmi kuwa kamwe kamwe wasakahifadhi hawataruhusiwa tena kukanyaga kwenye ardhi ya Uganda.

Amesema hayo saa chache baada ya kuthibitishwa kwa wagonjwa watano zaidi wa COVID-19 kando na tisa waliothibitishwa kwanzia usiku w aJumamosi wiki iliopita.

Hivyo Bwana Ecweru amesema hawawezi tena kuvumilia wakimbizi zaidi kuingia au kukaa nchini Uganda na kwa kutekeleza azimio hilo, wameanza kufunga mapokezi yote ya wakimbizi mpakani na mpakani na kisha kupunguza idadi ya waliokuwa tayari kwenye mapokezi ya wakimbizi makambini.

Akiongea akiwa mkali bwana Ecweru amesema si kw akuchukia wakimbizi lakini ni kwa kuhakikisha usalama wa Waganda na majirani zake.

Umauzi huo pia umetangazwa rasmi wakati ambapo wakimbizi 20 kutoka Jmahuri ya Kidemokrasia ya Kongo, (DRC) wameweka chini ya karantini ya siku 14 kuchunguzwa hali yao ya virusi vya COVID-19 wakiwa kwenye ufukwe wa Ziwa Albert wilayani Kagadi

Askari mmoja wa mpakani aliyetuhumiwa kuwatorosha kuingia nchini baada ya mpaka kufungwa amekamatwa na polisi.

Duniya Aslam Kahan Msemaji wa UNHCR, Uganda amesema kufuatia uamuzi huo, wameanza kuhamisha kwa dharura wasakahifadhi waliokuwa kwenye mapokezi ya wakimbizi kadi makambini.

Hata hivyo amesema msimamo wa UNHCR ni kuyaomba mataifa kuhakikisha wanatii haki za wakimbizi na makundi mengine yaliohatarini kwa kupunguz avikwazo mipakani na kuzingatia uhuru wa kutembea.

Wagonjwa wapya watano waliothibitishwa leo na Mkurugenzi Mkuu wa Huduma za Afya Henry Mwebesa ni raia wa Uganda watatu akiwemo mtoto mchanga mwneye umri wa miezi minane na Wachina wawili walioingia nchini wiki iliopita.