Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hatua zachukuliwa ili Ebola isienee nchi jirani na DRC

Uandaaji wa chanjo ya ebola katika maabara hospitali ya Donka, Conakry, Guinea
WHO/S. Hawkey
Uandaaji wa chanjo ya ebola katika maabara hospitali ya Donka, Conakry, Guinea

Hatua zachukuliwa ili Ebola isienee nchi jirani na DRC

Afya

Shirika la afya duniani WHO, limechukua hatua kuhakikisha ugonjwa wa Ebola uliolipuka huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC hauingii katika nchi 9 jirani na taifa hilo.

Nchi hizo ni Angola, Burundi, Jamhuri ya Afrika ya Kati, DRC, Jamhuri ya Congo, Rwanda, Sudan Kusini, Tanzania, Uganda na Zambia.

Taarifa ya WHO inasema kuwa usaidizi huo unalenga kuimarisha mifumo ya afya ili kuhakikisha iko katika hali ya kuweza kukabiliana na Ebola iwapo utaripotiwa katika nchi hizo.

HATUA PENDEKEZWA

Hatua kama vile kuchunguza, kukinga na kutibu Ebola ndio zinapatiwa msisitizo wakati huu ambapo tayari watu 37 wameripotiwa kufarika kwa Ebola huko DRC kati ya visa 57 vilivyoripotiwa.

Kwa mantiki hiyo WHO inataka mataifa hayo 9 yatathmini  uwezo wao wa sasa wa kukabiliana na mlipuko wa Ebola, yabaini upungufu uliopo na hatua zichukuliwe ili kuhakikisha uwezo wa kukabili upo.

Nchi hizo zinaelekezwa mazingira na vifaa vinavyopaswa kuwepo pindi kisa cha kwanza cha Ebola kinaporipotiwa na utayari wa kuendelea kufuatilia.

BAJETI

Kupitia mpango huo WHO itafanya kazi kwa karibu na wizara za afya na wadau wengine ambapo bajeti inayokadiriwa kwa maandilizi hayo kwa miezi tisa ni dola milioni 15.5

Mahitaji ya kila nchi ikiwemo utaalamu wa kiufundi na usaidizi mwingine utatolewa na ofisi za kikanda za WHO pamoja na makao makuu huko Geneva, Uswisi.

TAGS: WHO, Ebola, Tanzania, Uganda, DRC