Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNHCR yanusuru wakimbizi 74 waliokuwa wanashikiliwa Libya

Wakimbizi waliokuwa wanashikiliwa Libya. Picha: UNHCR

UNHCR yanusuru wakimbizi 74 waliokuwa wanashikiliwa Libya

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR limefanikiwa kuwahamisha wakimbizi 74 waliokuwa wanashikiliwa huko Libya na kuwasafirisha hadi Niger.

Hatua hiyo inafuatia matukio ya hivi karibuni yaliyokumba wakimbizi na wahamiaji ikiwemo kufanyika ukatili na kuuzwa utumwani wakati wakisaka hifadhi Ulaya.

Zoezi hilo linalosimamiwa na UNHCR na washirika limewezeshwa  kufuatia makubaliano ya Umoja wa Mataifa, Muungano wa Ulaya, Muungano wa Afrika ambapo  Alessandra Morelli, ambaye ni mwakilishi maalum wa UNHCR  Niger akiwa uwanja wa ndege kwa ajili ya mapokezi amesema….

(Sauti ya Alessandra Morelli)

“Tupo hapa  katika uwanja wa ndege ya Niamye tukisubiri ndege ya pili yenye kundi ya wakimbizi kutoka Eritrea waliookolewa kutoka korokoroni Libya . Kuna  wakimbizi 74  ambapo wengi wao ni watoto wasio na wazazi au walitengwa na wazazi wao. Niger ni kituo cha mpito, wanakaribiswa na pia watapatiwa huduma ipasavyo kadri ya uwezo wetu.”

Kwa msaada wa UNHCR  na washirika, wakimbizi kutoka  Somalia na Eritrea huko Niger, watapatiwa huduma muhimu kama makazi, chakula na huduma ya kisaikolojia wakati wakisubiri hatua ya kutafutiwa ifadhi ya kudumu.