Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

OHCHR yaorodhesha ukiukwaji wa haki za binadamu Eritrea

OHCHR yaorodhesha ukiukwaji wa haki za binadamu Eritrea

Nasikitika kuripoti kwamba Eritrea haijafanya jitihada zozote za kukomesha ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu ambao uchunguzi umebaini kuwa ni sawa na  uhalifu dhidi ya ubinadamu, amesema leo Mtaalamu Huru wa Haki za Binadamu nchini humo.

Bi. Sheela Kitharuth amesema mateso wanayoyapitia raia hao ni pamoja na kukamatwa kiholela, kuwekwa mahabusu bila mawasiliano, kutoweka na mfumo wa huduma za kitaifa ulio sawa na utumwa.

Ameongeza kuwa  hadi sasa mamlaka ya nchi hiyo imekataa kuonana naye kwa mwaka mmoja sasa, vile vile imekataa kuwaruhusu wataalamu wa kimataifa kufanya tathmini kuhusu ukiukwaji huo, akisema ufuatiliaji wa mbali ndio njia pekee ya kuangaza mwanga katika nchi ambayo inajificha kuchunguzwa.

Halikadhalika amesema mbali na mashirika ya kiserikali, Eritrea bado haina katiba, hakuna mfumo imara wa utawala wa kisheria, hakuna mahakama huru, bunge la kidemokrasia au baraza la kisheria, vyama vya upinzani, vyombo huru vya habari na mashirika ya kisheria.