Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mkutano wa bahari umefanikiwa, lakini kazi itaendelea:UM

Mkutano wa bahari umefanikiwa, lakini kazi itaendelea:UM

Siku tano zilizoghubikwa na mikutano, mijadala na vikao takribani 150 na maonyesho 41 katika mkutano wa kimataifa wa bahari kwenye makao makuu ya umoja wa Mataifa hapa New York hatimaye zimefunga mlango hii leo ijumaa.

Mkutano huo wa bahari uliowaleta pamoja wadau mbalimbali zaidi ya 1000, zikiwemo nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa, watalaamu wa sanyasi, mashirika ya kimataifa na asasi za kiraia, na ulijikita katika mada mbalimbali zinazohusu lengo nambari 14 la maendeleo endelevu , maisha chini ya maji.

Kikubwa kimekuwa ni kuangalia uhifadhi, matumizi endelevu ya bahari na rasilimali zake, changamoto na suluhu.

image
Isabella Lövin, waziri wa maendeleo ya kimataifa na mabadiliko ya tabia nchi wa Sweeden akihutubia washirki wa mkutano wa masuala ya bahari. Picha: UM
Washiriki wa mkutano huu wametoa ahadi ya kuchukua hatua kuhakikisha mustakhbali wa bahari hautofaidi kizazi hii pekee bali hata vijavyo. Mkutano huu umeendeshwa na Umoja wa Mataifa, serikali ya Fiji na Sweeden, Isabella Lövin ni waziri wa maendeleo ya kimataifa na mabadiliko ya tabia nchi wa Sweeden

(SAUTI YA ISABELLA)

“Hali ya bahari ni mbaya, ya kusikitisha na pia kutia hofu, na inatuathiri sote na mkutano huu wa bahari umekuwa ni fursa yetu ya kubadili ukurasa, huu ni mwanzo na hakuna kurudi nyuma na naamini utashi wa kisiasa uliodhihirika wiki hii, pengine ndio matokeo muhimu zaidi wiki hii, na sasa kibarua kigumu kinaendelea.”

image
Katibu mkuu wa mkutano huo Wu Hongbo (kati). Picha: UN Photo/Kim Haughton
Katibu mkuu wa mkutano huo Wu Hongbo akizunguza kwa niaba ya Umoja wa Mataifa katika mkutano na waandishi wa habari baada ya kufungwa kwa mkutano amesema Umoja wa Mataifa utashirikiana na wadao wote kufanikisha ajenda ya bahari

(SAUTI YA WU)

“Tuko tayari kusaidia nchi wanachama na wadau wengine katika mchakato unaofuata kwa kupitia uchambuzi na uwezeshaji , kubadilisha uzoefu na yale tuliyojifunza”

image
Rais wa baraza kuu Peter Thomson(kushoto). Picha: UN Photo/Evan Schneider
Naye rais wa baraza kuu Peter Thomson aliyekuwa mwenyeji wa mkutano huo amesema walichokitarajia wamekipata

(SAUTI YA THOMSON)

"Nimeridhika kwa asilimia 100, tulichokitaka kwenye mkutano huu tumekipata, na kitu kimoja nilicho na uhakika nacho kutoka kwenye mkutano huu na kuendelea hakuna mtu atakayesema hatukufahamu hali ilikuwa mbaya kiasi gani, hatukujua kwamba kutakuwa na maplastiki mengi baharini kuliko samaki ifikapo 2050, kiwango cha uelewa wa matatizo baharini kimepandishwa."