Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

FAO yatoa tahadhari dhidi ya virusi vinavyoathiri samaki aina ya sato au Tilapia

FAO yatoa tahadhari dhidi ya virusi vinavyoathiri samaki aina ya sato au Tilapia

Maradhi hatari yanayoambukiza yanasambaa miongoni mwa samaki aina ya sato au tilapia, moja ya samaki muhimu kwa matumizi ya binadamu. Flora Nducha na taarifa kamili

(TAARIFA YA FLORA)

Tahadhari hiyo imetolewa na shirika la chakula na kilimo FAO Ijumaa likisema mlipuko wa maradhi hayo uchukuliwe kwa tahadhari na nchi zinazosafirisha sato zihakikishe zimechukua hatua madhubuti za kudhibiti hatari kwa kuimarisha upimaji , kusisitiza hati za afya, kuchukua hatua za kuarantini na kujiweka tayari na mipango ya dharura.

Kwa mujibu wa kitengo cha FAO cha habari na mfumo wa tahadhari ya mapema kilichotoa tangazo hilo , virusi hivyo viitwavyo Tilapia Lake Virus (TiLV) sasa vimeshathibitishwa katika nchi tano kwenye mabara matatu duniani ambazo ni Colombia, Ecuador, Misri, Israel na Thailand.

FAO inasema ingawa kwa sasa virusi hivyo havina hatari yoyote kwa afya ya binadamu , vinauwezekano mkubwa wa kuathiri uhakika wa chakula na lishe duniani. Mwaka 2015 biashara ya sato duniani ilikadiriwa kuwa na thamani ya dola bilioni 1.8.