Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Idadi ya wasio na chakula duniani yaongezeka- Ripoti

Idadi ya wasio na chakula duniani yaongezeka- Ripoti

Ripoti mpya kuhusu hali ya janga la chakula duniani imesema idadi ya watu wasio na uhakika wa kupata chakula iliongezeka mwaka jana na kufikia watu milioni 108, ikilinganishwa na milioni 80 mwaka 2015, licha ya jitihada za kimataifa za kuhakikisha watu wana chakula cha kutosha. Taarifa kamili na Flora Nducha.

(Taarifa ya Flora)

Ikiwa imeandaliwa na mashirika ya Umoja wa Mataifa kama lile la chakula, FAO na wadau wao ukiwemo Muungano wa Ulaya na shirika la maendeleo ya kimataifa la Marekani, USAID, ripoti imetolewa leo huko Brussels, Ubelgiji ikisema idadi hiyo inagusa tu watu ambao hali zao ziko taabani zaidi.

Kichocheo kikubwa cha ukosefu wa chakula ni mizozo ambapo ripoti imesema kuwa nchi 10 kati ya 13 zinazokabiliwa na njaa ya kupindukia ni zile zenye migogoro kama vile Somalia, Sudan Kusini na Nigeria.

Luca Russo, mshauri mwandamizi kutoka FAO amesema ripoti hii ni muhimu sana kwa kuwa imejumuisha mashirika yote yanahusika na usaidizi kwenye janga la chakula na hivyo..

(Sauti ya Luca)

“Kuna idadi tofauti tofauti ya watu wanaokabiliwa na uhaba wa chakula, watu wakitumia mbinu tofauti kukusanya taarifa na mashirika tofauti. Lakini ripoti hii ni muhimu kwa kuwa inatokana na makubaliano baina ya mashirika yote yanayohusika na janga la chakula, kitu ambacho ni muhimu katika uamuzi.” 

Ripoti inaeleza kuwa muda unasonga na hivyo jamii ya kimataifa ichukue hatua kuokoa maisha ya mamilioni ya watu walio kwenye hatari ya kukumbwa na njaa.