Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban ajadili na Rais wa Ufaransa kuhusu sintofahamu inayoendelea CAR

Ban ajadili na Rais wa Ufaransa kuhusu sintofahamu inayoendelea CAR

Hali inayoendelea hivi sasa huko Jamhuri ya Afrika ya kati ni ya kusikitisha na imesababisha  udharura unaokumba wananchi wote hususan wanawake na watoto, amesema Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon katika mazungumzo yake kwa simu na Rais wa Ufaransa François Hollande.

Bwana Ban ameelezea wasiwasi zaidi juu ya ongezeko la mzozo kwa misingi  ya kidini na kijamii wakati huu ambapo Umoja wa Mataifa tayari umetuma maafisa wa  haki za binadamu kufuatialia ghasia zinazoendelea nchini humo dhidi ya raia na kuandaa mazingira ya kupeleka ujumbe wa kudumu kuhusu haki za binadamu mapema mwakani.

Halikadhalika Ban na Rais Hollande wamezungumzia jitihada zinazoendelea za kusaidia ujumbe wa Afrika wa kulinda amani nchini Jamhuri ya Afrika  ya Kati, MISCA wakizingatia umuhimu wa kuimarisha uwezo wake kwa kuongeza idadi ya askari wa kuimarisha usalama, kupokonya silaha na kusaidia maandalizi ya uchaguzi.

Kufuatia ombi la Baraza la Usalama, tayari Umoja wa Mataifa umeanza mipango ya uwezekano wa kubadili MISCA kuwa operesheni yake ya ulinzi wa amani. Hata hivyo mashauriano zaidi ya haraka kuhusu sualahiloyatafanyika siku chache zijazo.