Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban asema Syria suala la Syria lilishika kasi zaidi mwaka 2013

Ban asema Syria suala la Syria lilishika kasi zaidi mwaka 2013

Wakati tunapohesabu siku chache kabla ya kuhitimisha mwaka, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon, LEO amekutana na waandishi wa habari kuzungumzia mwaka 2013. Miongoni mwa mambo aliyoangazia ni amani na usalama, huku suala la mzozo wa Syriabado  likitawala, kama ilivyokuwa mwaka ulopita.

“Mwaka 2013 ndio mwaka ambao mzozo wa Syria ulikithiri kwa kiwango kisichofikirika.Watu wa Syria hawawezi kuhimili mwaka mwingine, mwezi mwingine au siku nyingine ya ukatili na uharibifu. Nimelihutubia Baraza la Usalama kuhusu ripoti ya uchunguzi wa timu iloongozwa na Profesa Ake Sellstrom. Tunapaswa kusikitishwa na matokeo yake kuwa silaha za kemikali zilitumiwa, siyo tu Agosti Ghouta karibu na Damscus, lakini pia mara nyingine kadhaa, dhidi ya raia”

Barani Afrika, Bwana Ban ameangazia hali ukanda waSahel, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo na Jamhuri ya Afrika ya Kati

(BAN)

“Mwaka 2013 ndio ambao jamhuri ya Afrika ya Kati ilitumbukia katika machafuko. Nahofia sana tishio la janga linaloweza kuathiri halaiki ya watu. Natoa wito kwa mamlaka za mpito nchini humo kuwalinda watu. Natoa wito kwa viongozi wa kidini na kijamii kuzuia uenezaji wa chuki. Nakaribisha kupelekwa kwa vikosi vya Afrika na Ufaransa ambavyo tayari vinaleta mabadiliko.”

Bwana Ban pia amemulika picha ya kazi ya mwaka ujao wa 2014

(BAN)

“Ni lazima tuufanye mwaka 2014 mwaka wa kuwalinda watu- usalama wao, haki zao za msingi na maslahi yao. Mwaka 2013 utakumbukwa kama mwaka tuliompoteza Nelso Mandela. Siwezi kuwazia chochote kingine ambacho ningependa kuona mwaka 2014, isipokuwa viongozi duniani kuiga mfano wa Mandela katika kutekeleza wajibu wao wa kimaadili na kisiasa.”