Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Maafisa wakuu wa Umoja wa Mataifa waitaka Syria kuwalinda wahudumu wa afya

Maafisa wakuu wa Umoja wa Mataifa waitaka Syria kuwalinda wahudumu wa afya

Wahudumu wa afya nchini Syria ni lazima walindwe, wamesema maafisa wa ngazi ya juu wa masuala ya kibinadamu katika Umoja wa Mataifa, huku wakitoa wito kwa mara nyingine kwama vituo vya afya vipewe ulinzi ili raia waweze kupata dawa za matibabu na chanjo na usaidizi mwingine muhimu wa kibinadamu. Maafisa hao, wakiwemo Mratibu Mkuu wa masuala ya kibinadamu, OCHA, Valerie Amos, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Duniani, WHO, Margaret Chan na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Kuhudumia Watoto,UNICEF, Anthony Lake wamesema hayo katika taarifa ilotolewa miwshoni mwa wiki. Katika taarifa hiyo ya pamoja, maafisa hao wamelaani vikali mashambulizi dhidi ya vituo vya afya na vituo vingine vya umma, na kusema kuwa wamesikitishwa mno na madhara yake kwa wagonjwa, wahudumu wa afya na utoaji wa huduma na vifaa muhimu vya afya. Zaidi ya asilimia 60 ya hospitali za umma hazifanyi kazi nchini Syria, huku idadi sawa ya magari ya kuwasafirisha wagonjwa hospitali yakiwa yameharibiwa au kuibiwa, kwa mujibu wa takwimu za Umoja wa Mataifa. Wakuu hao wa mashirika ya Umoja wa Mataifa wamesema kuwa mashambulizi dhidi ya vituo vya afya yanaweza kuchukuliwa kama uhalifu wa kivita chini ya sheria ya kimataifa.