Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabia nchi kunahitaji hatua za mapema

Kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabia nchi kunahitaji hatua za mapema

Shirika la mpango wa chakula duniani FAO limesema kuwa kuchukuliwa kwa hatua za mapema pamoja na uwekezaji wa kutosha ni mambo yanayohitajika ili kukabiliana na kitisho cha mabadiliko ya tabia kinachokabili misitu duniani. George Njogopa na taarifa zaidi.

(Taarifa ya George)

Katika taarifa yake iliyotoa mwongozo kuhusiana na uangalizi wa misitu, FAO imesema kuwa dunia inaweza kuzikwepa gharama kubwa iwapo itawajibika kuchukua jukumu la kuzifanyia marekebisho sera zake kuhusiana na misitu, lakini kama itashindwa kufanya hivyo athari za kukabiliana na mathara yatayojitokeza ni kubwa.

Imebainisha pia faida ambazo dunia itajivunia ni pamoja na na kuboresha ustawi wa watu wake na kuwa na uhakika wa usalama wa chakula

Afisa wa FAO Simmone Rose amesema kuwa suala la tabia nchi ni suala tete ambalo linaathiri mfumo mzima wa viumbe hai vilivyoko baharini na nchi kavu.

Amesema  mwongozo huo uliotolewa unatazamia kutoa faida kubwa ikiwemo ile ya kuwezesha kufanyika tathmini na baadaye usimamizi juu ya matokeo yatokanayo na mabadiliko ya tabia nchi.

Mwongozo huo unafahamisha hatua zinazopaswa kufuatwa wakati wa kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabia nchi. Pia inahimiza kile kinachoitwa usimamizi sahihi kuhusiana na uhifadhi wa mazingira.