Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban asikitishwa na kinachoendelea Misri, ataka mamlaka na wanasiasa kunusuru nchi

Ban asikitishwa na kinachoendelea Misri, ataka mamlaka na wanasiasa kunusuru nchi

Katibu Mkuu wa Umoja wa mataifa Ban Ki Moon amesema anatiwa hofu na hali ya usalama inavyozidi kuzorota nchini Misri pamoja na kuenea kwa ghasia na matumuzi ya nguvu kupita kiasi dhidi ya waandamanaji. Taarifa ya msemaji wa Umoja wa Mataifa iliyotolewa Jumamosi imemkariri Bwana Ban akishutumu vikali mashambulio dhidi ya makanisa, hospitali na maeneo mengine ya umma, jambo ambalo amesema anaona halikubaliki. Amesema licha ya machungu yoyote hakuna cha kuhalalisha uharibifu wa miundombinu na mali ambazo ni muhimu kwa hatma ya Misri. Bwana Ban amesema anaamini kuwa kuzuia vifo zaidi kunapaswa kuwa kipaumbele kikubwa cha Misri wakati huu wa hatari. Amewasihi waandamanaji na mamlaka  kujizuia huku akitaka mamlaka na viongozi wa kisiasa kuibuka na mpango wa kuleta utulivu na kupeleka mbele mchakato wa kisiasa uliositishwa na ghasia. Katibu mkuu amesema wakati wote mchakato wa kisiasa husonga mbele na kamwe haurudi nyuma hivyo ametaka wamisri wote kumaliza tofauti zao kwa amani kwani hali ilivyo sasa mamlaka na wanasiasa wanawajibika.