Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mashirika ya misaada yajipanga kutathmini hali halisi CAR

Mashirika ya misaada yajipanga kutathmini hali halisi CAR

Wakati ripoti zikieleza kuwepo kwa mazungumzo kati ya serikali ya Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR na waasi, mratibu wa misaada ya kibinadamu nchini humo Dkt. Zakaria Maiga amesema wanajiandaa kupeleka jopo la kutathmini hali ya mahitaji kwenye maeneo yaliyokumbwa na mzozo nchini humo.Taarifa zaidi na Jason Nyakundi.

Afisa huyo ametoa kauli hiyo wakati huu ambapo vikundi vya misaada vinakabiliwa na changamoto kuweza kusambaza mahitaji muhimu kwa wananchi ambapo waasi wa kikundi kiitwacho SELEKA wameshikilia baadhi ya miji.

Dkt. Zakaria Maiga wa OCHA amesema wana wasiwasi kuwa mzozo huo utaathiri usambazaji wa misaada ya kibinadamu na kwamba wana imani kuwa mahitaji makubwa yatakuwa ni ya ulinzi wa raia, msaada wa kijamii na ushauri nasaha ili kukabiliana na msongo wa akili kwa waliojikuta katikati ya mzozo huo baina ya serikali na waasi.

Hata hivyo ametaka pande zote kuhakikisha wanaruhusu misaada ya dharura ya kibinadamu inasambazwa kwa raia bila vizuizi vyovyote.

Takribani asilimia Saba ya wananchi wote Milioni Nne na Laki Sita wa Jamhuri ya Afrika ya Kati wanaishi kwenye eneo lenye mapigano nchini humo.