Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Baraza la Usalama limechukua hatua madhubuti kulinda tembo: CITES

Baraza la Usalama limechukua hatua madhubuti kulinda tembo: CITES

Mtendaji Mkuu wa Mkataba wa kimataifa wa udhibiti wa biashara ya viumbe vilivyo hatarini kutoweka, CITES, John Scanlon amesifu wito wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa wa kutaka uchunguzi dhidi ya madai kuwa waasi wa kikundi cha LRA wanaua tembo na kuuza meno yao kimagendo.

Bwana Scanlon amesema hatua hiyo ni ya kihistoria na inalenga kupatia suluhu wasiwasi uliowahi kujitokeza juu ya uhusiano kati ya biashara haramu ya wanyamapori na usalama barani Afrika.

Amesema sekretarieti ya CITES iko tayari kushirikiana na washirika wake kuchunguza uhusika wa waasi hao na uhalifu dhidi ya wanyamapori hususan tembo.

Wiki iliyopita, taarifa ya Rais wa Baraza la usalama ilitaka Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika kushirikiana kuchunguza madai kuwa vyanzo vya mapato vya LRA ni pamoja na biashara haramu ya meno  ya tembo.