Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kazi ya kujitolea imesaidia kutekeleza Malengo ya Milenia: Ban

Kazi ya kujitolea imesaidia kutekeleza Malengo ya Milenia: Ban

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon ametoa ujumbe wake wa siku ya kimataifa ya kujitolea hii leo na kusema kuwa kazi inayofanywa na wafanyakazi wa kujitolea inasaidia kufanikisha malengo ya maendeleo ya milenia ya mwaka 2015.

Katika ujumbe wake Bwana Ban amesema wafanyakazi hao wakiwemo 7,700 wa Umoja wa Mataifa wameshiriki kazi mbali mbali ikiwemo kuzuia mapigano, harakati za kuondokana na umaskini, kuendeleza maendeleo endelevu na miradi kadhaa ya kuboresha maisha.

Ameongeza kuwa ni matumaini yake kuwa wafanyakazi hao wataendelea na moyo huo huo wa kujitolea katika kutekeleza ajenda ya maendeleo baada ya mwaka 2015.

Bwana Ban amehusisha pia maendeleo ya teknolojia ya mawasiliano na kujitolea ambapo amesema mtu yeyote mwenye mtandao wa intaneti kwa sasa au simu ya mkononi anaweza kuleta mabadiliko bora ya maisha ya wengine.

Amesema katika maadhimisho ya siku ya kimataifa ya kujitolea, kila mtu ajizatiti kutumia uwezo na matarajio yake kusaidia wengine kwa njia ya kujitolea.