Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Twasubiri kwa hamu ziara ya Baraza la Usalama Sudan Kusini- Loej

Twasubiri kwa hamu ziara ya Baraza la Usalama Sudan Kusini- Loej

Mkuu wa Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini, UNMISS  Bi Ellen Margaret Loej amesema ziara ya  Baraza la Usalama itakayoanza nchini humo kesho Jumamosi, itawapa fursa ya kuona changamoto zinazowakabili watu wa Sudan Kusini hususan wale walio ndani ya kituo cha ulinzi wa raia.

Akihojiwa na Radio Miraya iliyo chini ya UNMISS, amesema anatarajia watakuwa na mazungumzo na vikundi vya kiraia ili kupata picha halisi kuhusu hali ya usalama, haki za binadamu na changamoto zingine zinazokumba raia.

Halikadhalika watapata fursa ya kusikia kutoka serikali ya mpito kuhusu wasiwasi ama changamoto zao katika kupata msaada kutoka UNMISS, utekelezaji wa mamlaka mpya za ujumbe huo pamoja na mkataba wa amani.

image
Mwakilishi maalum wa Katibu Mkuu wa UM huko Sudan Kusini na mkuu wa UNMISS Ellen Margrethe Loej. (Picha:UN/JC McIlwaine)
Bi. Loej ameongeza kuwa Baraza la Usalama limekuwa na wasiwasi mkubwa na

(Sauti ya Ellen)

"Baraza la usalama, kama ilivyo kwetu sisis hapa, limekuwa na wasiwasi mkubwa juu ya kuendelea kwa mapigano katika maeneo mbalimbali ya nchi. Tuna wasiwasi na  hali ya usalama na ya kibinadamu , hivyo ni matumaini yetu kuwa ziara hii itatoa msukumo wa majadiliano ya wazi, juu ya namna bora serikali na Umoja wa Mataifa wanaweza kufanya kazi pamoja kwa manufaa ya watu wa Sudan Kusini."

 Bi. Loej amesema ziara hiyo ya siku tatu Sudan Kusini inakuja wakati muafaka ambapo wanakaribia kuwasilisha ripoti ya UNMISS kwa Katibu Mkuu.

Kutoka Sudan Kusini, wajumbe wa Baraza la Usalama wataelekea Addis Ababa, Ethiopia kwa mazungumzo  tarehe Tano Septemba na Muungano wa Afrika kabla ya kurejea New York, Marekani.