Hadhi mpya ya Palestina ndani ya Baraza Kuu la UM kuchochea amani Mashariki ya Kati
Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa siku ya Alhamisi tarehe 29 Novemba ambayo ni siku ya kimataifa ya kusimama bega kwa bega na Palestina, lilipitisha azimio la kuipatia Palestina hadhi ya uangalizi bila haki ya kupiga kura katika Baraza hilo.
Katika kura hiyo ya kupitisha azimio hilo, nchi 138 ziliunga mkono huku Tisa zikipinga na nchi 41 zikiwa hazikuonyesha msimamo wowote. Nchi zilizopiga kura ya hapana ni pamoja na Marekani na Israeli huku Uingereza na Hungary zikiwa miongoni mwa nchi ambazo hazikuonyesha msimamo wowote.