Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Licha ya yale “makubaliano ya Istanbul ya kuvusha nafaka”, hakuna matarajio ya kumalizika vita Ukraine 

Rosemary DiCarlo, Msaidizi wa Katibu Mkuu UN katika Masuala ya Kisiasa na Kujenga Amani, akitoa maelezo kwa wajumbe wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuhusu hali ya Ukraine. Julai, 29, 2022
UN Photo/Mark Garten
Rosemary DiCarlo, Msaidizi wa Katibu Mkuu UN katika Masuala ya Kisiasa na Kujenga Amani, akitoa maelezo kwa wajumbe wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuhusu hali ya Ukraine. Julai, 29, 2022

Licha ya yale “makubaliano ya Istanbul ya kuvusha nafaka”, hakuna matarajio ya kumalizika vita Ukraine 

Amani na Usalama

Umoja wa Mataifa una wasiwasi mkubwa kuhusu kukosekana kwa matarajio ya kuanza tena kwa juhudi za kidiplomasia za kumaliza vita nchini Ukraine. Amesema leo Mkuu wa Idara ya siasa kwenye Umoja wa Mataifa Rosemary DiCarlo, akizungumza katika Baraza la Usalama jijini New York Marekani. 

"Vitisho vya upanuzi wa kijiografia wa mzozo na kunyimwa haki ya utaifa kwa haviendani na ari ya mazungumzo ya Istanbul kuhusu nafaka.” Amesema Bi DiCarlo.  

Katika hotuba yake, Bi. DiCarlo ameielezea hali ya Ukraine kama "hali ngumu ya kibinadamu na inayozidi kuzorota nchini Ukraine": vifo vya raia, mamilioni ya wakimbizi, uharibifu mkubwa wa miundombinu ya raia na miundombinu ya kitamaduni. 

Ukraine kwenye moto 

Kharkiv, Dnipro, Nikolaev, miji ya Donbass, mji mkuu wa eneo la Kirovogad na makazi mengine yanashambuliwa. Baadhi ya miji ya Ukraine imeharibiwa kabisa. Kwa mujibu wa Ofisi ya Kamishna Mkuu wa Haki za Kibinadamu wa Umoja wa Mataifa, hadi kufikia Julai 27, raia 5,237 waliuawa na 7,035 walijeruhiwa nchini Ukraine. "Hizi ni takwimu zilizothibitishwa tu, iadi halisi ni kubwa zaidi," Rosemary DiCarlo amesema akiongeza kuwa  vifo vingi vinasababishwa na matumizi ya silaha za milipuko ya masafa mapana katika maeneo yenye watu wengi. 

Mashambulizi kwenye vituo vya afya pia yanatia wasiwasi sana Umoja wa Mataifa. Kufikia Julai 25, kulikuwa na mashambulizi 414 kama hayo, ambayo yalisababisha vifo vya watu 85 na wengine 100 kujeruhiwa. Vitu 168 vya muhimu wa kitamaduni viliharibiwa, zikiwemo taasisi 73 za kidini na makumbusho 13. Kutokana na mashambulizi hayo, taasisi 2,129 za elimu ziliharibiwa. "Mashambulizi ya kiholela dhidi ya raia na miundombinu ya kiraia ni wazi kuwa ni ukiukaji wa sheria za kibinadamu na sheria za haki za binadamu," ameonya Bi. DiCarlo akiongeza kwa kusema, "tunahimiza pande zote (katika mzozo) kuheshimu sheria." 

Ukraine inakumbwa na uharibifu mkubwa wa miundombinu ambao utagharimu fedha nyingi kukarabati au kujenga upya.
© UNDP/Oleksandr Ratushniak
Ukraine inakumbwa na uharibifu mkubwa wa miundombinu ambao utagharimu fedha nyingi kukarabati au kujenga upya.

Msaada kutoka UN 

Akigusia suala la usaidizi wa kibinadamu wa Umoja wa Mataifa, amekumbushia kuwa tangu Februari 24, Waukraine milioni 11 wamepata msaada, milioni tisa kati yao katika sekta ya chakula. Zaidi ya milioni nne wamesaidiwa kupata maji safi, na zaidi ya milioni mbili wamepata msaada wa kifedha. 

Licha ya ugumu wa kufikisha misaada ya kibinadamu katika maeneo ya mikoa ya Donetsk na Lugansk isiyodhibitiwa na serikali ya Ukraine, wadau wa masuala ya kibinadamu wa Umoja wa Mataifa waliweza kutoa msaada kwa wakazi 125,000 wa ndani, pamoja na taasisi 30 za afya, elimu na ulinzi wa kijamii. 

Wakimbizi na wakimbizi wa ndani 

Kufikia Julai 19, idadi ya wakimbizi kutoka Ukraine ilifikia watu 5,984,263 barani Ulaya. Kwa jumla, tangu Februari 24, watu milioni 9.5 wameondoka Ukraine, na milioni 3.8 wamevuka mpaka kuingia Ukraine. 

Umoja wa Mataifa una wasiwasi mkubwa kwamba majira ya baridi kali yanapokaribia, wakimbizi wa ndani na waliorejea nyumbani Ukraine watakabiliwa na matatizo ya ziada yanayohusiana na makazi yenye joto na upatikanaji wa huduma za matibabu. Umoja wa Mataifa na washirika, kulingana na DiCarlo, wanajaribu kuzuia matatizo haya. 

Wakimbizi kutoka Ukraine wakiingia Poland baada ya kuvuka mpaka katika kituo cha mapakani cha Medyka.
© UNHCR/Maciej Moskwa
Wakimbizi kutoka Ukraine wakiingia Poland baada ya kuvuka mpaka katika kituo cha mapakani cha Medyka.

Hali ya wanawake 

Katika hotuba yake, kiongozi huyo amefafanua pia hali ya wanawake. Kwa mfano, amesema kaya zinazoongozwa na wanawake zina uwezekano mara mbili wa kupata uhaba wa chakula kuliko kaya zinazoongozwa na wanaume. Afya ya uzazi, huduma ya matibabu kwa watoto, elimu ya nyumbani ya watoto na hii ni orodha isiyo kamili ya matatizo ambayo wanawake wa Ukraine wanakabiliwa nayo kuitatua. 

Aidha, ripoti za unyanyasaji wa kijinsia, ikiwa ni pamoja na madai ya unyanyasaji wa kijinsia unaohusishwa na migogoro, zinaongezeka, na huduma za usaidizi wa waathirika haziwezi kutoa msaada unaohitajika. Uwezekano mkubwa zaidi, waathiriwa wengi hawawezi kupata msaada. DiCarlo amependekeza. 

"Kuhusiana na hayo yote hapo juu, ni muhimu sana kwamba wanawake washiriki katika mijadala ya mipango ya mustakabali wa nchi, ikiwa ni pamoja na mazungumzo ya amani, juhudi za ujenzi mpya, ujenzi wa amani na uwajibikaji (kwa uhalifu uliofanywa)." DiCarlo amesisitiza. 

Matarajio ya suluhu ya kidiplomasia 

Licha ya matokeo chanya ya mazungumzo ya nafaka na mbolea, Umoja wa Mataifa una wasiwasi mkubwa juu ya kukosekana kwa matarajio yoyote ya kurejesha juhudi za kidiplomasia zenye lengo la kumaliza vita.  

Pia ameonesha kusikitishwa na ripoti za juhudi za kubadilisha muundo wa utawala katika maeneo yasiyodhibitiwa na serikali, pamoja na majaribio ya kuanzisha serikali za mitaa katika maeneo yanayodhibitiwa na Urusi. Kwa mujibu wake, vitendo kama hivyo vinaleta wasiwasi mkubwa juu ya matokeo ya kisiasa ya vita.