COVAX yawasilisha dozi zaidi ya 350,00 za chanjo ya COVID-19 Niger
COVAX yawasilisha dozi zaidi ya 350,00 za chanjo ya COVID-19 Niger
Serikali ya Niger leo imepokea Zaidi ya dozi 350,000 za chanjo dhidi ya corona au COVID-19 kupitia mkakati wa kimataifa wa kuhakikisha kila nchi inapata chanjo unaosimamiwa na Umoja wa Mataifa COVAX.
Chanjo hizo za awali za AstraZeneca zitatumika kuwalenga zaidi wahudumu walio msitari wa mbele hasa wahudumu wa afya, waalimu, na watu ambao wako hatarini Zaidi kuambukizwa virusi vya corona.
Chanjo hizi zinasaidia makubaliano mengine ya nchi mbili na kupitia Muungano wa Afrika.
Makubaliano hayo yatasaidia chanjo kwa asilimia 20 ya idadi ya watu wote wanaopewa kipaumbele, yakiunga mkono mpango wa kitaifa wa chanjo unaosaidiwa na UN ambao unajumuisha wahamiaji na wakimbizi, pamoja na wahudumu wa misaada.
Louise Aubin, ambaye ni naibu mwakilishi maalum wa Katibu Mkuu, na mratibu mkazi na wa masuala ya kibinadamu, amesisitiza tena kujitolea kwa Umoja wa Mataifa kusaidia utoaji wa chanjo kote nchini hadi kinga ya pamoja itakapopatikana.
Shirika la afya la Umoja wa Mataifa WHO na na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia Watoto UNICEF, wanasaidia mamlaka kusimamia kitengo kikuu cha kuhifadhi takwimu za wapokeaji chanjo wanaostahiki, usimamizi wa chanjo na utambuzi wa maeneo ya chanjo, usafirishaji, uhifadhi na usambazaji, na huku timu nzima ikihamasishwa kuendelea kuzuia kuenea kwa COVID-19 na kuongeza kampeni za chanjo .