Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Heko serikali zilizochukua hatua za kijasiri na kuwezesha watoto kurejea shuleni - UNICEF

Mvulana mdogo akisafisha mikono yake wakati anaingia katikashule yake mjini Yambio, Sudan Kusini, Jumanne Machi 17, 2020
© UNICEF/UNI315623/Ongoro
Mvulana mdogo akisafisha mikono yake wakati anaingia katikashule yake mjini Yambio, Sudan Kusini, Jumanne Machi 17, 2020

Heko serikali zilizochukua hatua za kijasiri na kuwezesha watoto kurejea shuleni - UNICEF

Utamaduni na Elimu

Ugonjwa wa virusi vya Corona au COVID-19 ulipovuruga mwenendo wa elimu duniani, kila mtu alisalia na maswali mengi! Je tufanye vipi watoto waweze kuendelea kujifunza? Tufanye vipi ili kuhakikisha watoto wanapata msaada muhimu kupitia shule ikiwemo mlo wenye lishe?
 

Hayo ni maswali ambayo shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF pamoja na wadau walijiuliza kuanzia mwezi Machi mwaka huu COVID-19 ilipotangazwa kuwa janga la kimataifa.

Maswali yaliendelea, mfano! Kwa vipi shule zitafunguliwa tena huku usalama wa watoto ukipatiwa kipaumbele? 
Lakini baada ya muda, mambo mengi yamefahamika na UNICEF na wadau wake wamejifunza mambo mengi na kile cha kufanya.

Mkurugenzi Mtendaji wa UNICEF Henrietta Fore anataja mambo makuu manne ambayo serikali zinapaswa kuzingatia.

Mosi ni kutochangamana pamoja na usafi.

Ametoa mfano wa “nchini Senegal, shule zimehakikisha kuna kutochangamana miongoni mwa watoto kwa kuongeza nafasi kati ya mwanafunzi na mwanafunzi darasani. Serikali kuanzia Afghanistan hadi Albania zimeimarisha huduma za kunawa mikono na usafi shuleni na zimeweka kanuni za uchunguzi wa afya. Shule nyingi zimeachana na michezo ya ndani na sasa watoto wanacheza nje.”

Halikadhalika amesema shule zinahamasisha unawaji mikono ili kusaidia watoto wawe salama iwe shuleni au nyumbani.

Daniel Mungoci mwenye umri wa miaka 16 akiwa anajisomea nyumbani wakati huu ambapo bado shule zimefungwa nchini Uganda kutokana na COVID-19.
UNICEF/Francis Emorut
Daniel Mungoci mwenye umri wa miaka 16 akiwa anajisomea nyumbani wakati huu ambapo bado shule zimefungwa nchini Uganda kutokana na COVID-19.

Hatua ya pili ni ufundishaji unaoendana na hali halisi

Bi. Fore amesema, “nchi kama Misri, Namibia na Papua New Guinea zimeanzisha madarasa madogo na zimeongeza muda wa masomo ili kuhakikisha watoto wanasoma kwa zamu. Rwanda inajenga madarasa mapya na kuajiri walimu zaidi ili kuepusha msongamano darasani. Italia inaajiri walimu wa muda mfupi ili kusaidia kufundisha.”

Mkurugenzi Mtendaji huyo wa UNICEF amesema nchini nyingi zinatumia ufundishaji mchanganyiko ikimaanisha kwamba, “watoto wanafundishwa darasani na vile vile wakiwa nyumbani.”

Nchi zingine zimeondoa walimu kutoka katika majukumu ya hatari zaidi hadi majukumu yenye hatari kidogo.

Hatua ya tatu ni ufunguaij wa shule kwa awamu

Mataifa kama vile China, Indonesia na Uruguay yanachukua hatua kwa hatua katika ufunguaji wa shule zao.
“Mathalani, wanaweza kuanza na maeneo yenye hatari kidogo zaidi ya kupata COVID-19 au wakaanza na wanafunzi wadogo kwanza. Hii inatoa fursa ya kufanyia majaribio kanuni za usalama na kujumuisha wazazi, walimu na wanafunzi,” amesema Bi. Fore.

Wanafunzi katika shule ya msingi ya Preah Norodom mjini Phnon Penh nchini Cambodia wakati wa siku ya pili ya kufunguliwa kwa shule. Wanafunzi, walimu na mkurugenzi wa shule wanavaa barakoa wanapokuwa shuleni.
UNICEF/Seyha Lychheang
Wanafunzi katika shule ya msingi ya Preah Norodom mjini Phnon Penh nchini Cambodia wakati wa siku ya pili ya kufunguliwa kwa shule. Wanafunzi, walimu na mkurugenzi wa shule wanavaa barakoa wanapokuwa shuleni.

Hatua ya nne ni jinsi ya kufikia watoto walio hatarini zaidi

UNICEF inashirikiana na serikali ya Burkina Faso kuhamasisha kuhusu umuhimu wa elimu kwa mtoto wa kike wakati huu wa kampeni za kurejea tena shuleni.

“Inatia moyo sana kuona wanafunzi, wazazi, walimu na watunga sera wakichukua hatua za kukabili janga hili. Tunatiwa moyo pia na nchi kama Burundi, Uholanzi na Denmark. Hizi zimefungua shule bila kushuhudia ongezeko la maambukizi ya COVID-19, au ongezeko la kusambaa kwa virusi miongoni mwa wanajamii,” amesema Mkurugenzi Mtendaji huyo wa UNICEF.

Amesema kwa upande wao, Israel, Ufaransa na China, zilidhibiti haraka sana mlipuko wa Corona kwenye baadhi ya maeneo pindi tu taarifa zilipopatikana.

Ni kwa mantiki hiyo amesema kuwa UNICEF inaendelea kutoa wito kwa serikali kupatia kipaumbele suala la ufunguaji wa shule na zichukue hatua mujarabu kudhibiti maambukizi.

Amekumbusha kuwa kitendo cha shule kufungwa, kimekuwa na madhara mabaya sana kwa watoto ambapo watoto walio pembezoni ndio wameathirika zaidi.

“Sasa ni wakati wa kusaidia na kuwekezaji haraka kwenye elimu kwa kila mtoto,”  ametamatisha Bi. Fore.