Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watoto milioni 776 wakosa kuhudhuria shule kwa sababu ya COVID-19:UNESCO

Maonyesho ya darasa lisilokuwa na mwisho likiashiria hali ya janga la elimu duniani.
TheirWorld
Maonyesho ya darasa lisilokuwa na mwisho likiashiria hali ya janga la elimu duniani.

Watoto milioni 776 wakosa kuhudhuria shule kwa sababu ya COVID-19:UNESCO

Utamaduni na Elimu

Shirika la Umoja wa Mataifa la elimu, sayansi na utamaduni UNESCO limesema nchi 100 duniani zimefunga kabisa au kwa kiasi fulani shule na vituo vya elimu na kuwakosesha mamilioni ya watoto masomo, kwa sababu ya mlipuko wa COVID-19 unaoendelea.

Shirika hilo sasa linasema hivi sasa linazisaidia nchi kusaka suluhu ya jinsi ya watoto kuweza kusoma wakiwa nje ya mazingira ya shule ikiwemo kupitia mtandaoni na nyenzo zingine za kidijitali

Kwa mujibu wa UNESCO nchi 85 zimefunga shule katika nchi nzima ili kujaribu kudhibiti maambukizi ya virusi hivyo vipya vya Corona. Hatua hizo zimewaathiri watoto na vijana zaidi ya milioni 776.7.

Wanafunzi wakitumia kompyuta mpakato katika mraddi wa shule wa (INS) kwenye kambi ya wakimbizi ya Kakuma nchini Kenya. Mradi wa INS ni wa ushirikiano baina ya UNHCR na wakfu wa Vodafone.
UNHCR/Catherine Wachiaya
Wanafunzi wakitumia kompyuta mpakato katika mraddi wa shule wa (INS) kwenye kambi ya wakimbizi ya Kakuma nchini Kenya. Mradi wa INS ni wa ushirikiano baina ya UNHCR na wakfu wa Vodafone.

Matumizi ya teknolojia

Akizungumza na UN News kwa njia ya simu kutoka mjini Brussels nchini Ubelgiji mwakilishi wa UNESCO nchini humo Vincent Defourny amesema UNESCO inashirikiana kwa karibu na serikali ili kutekeleza mapendezo ya matumizi ya teknolojia.

“UNESCO inashauri kupunguza athari kwa mitaala ya shule kwa njia mbalimbali. Kitu cha kwanza ni kutumia rasilimali zote zilizopo za kuwezesha kusoma wakiwa mbali ambazo zinaweza kuwa ni kupitia mtandao wa intaneti, radio, televisheni na njia zingine zote zinazoruhusu kusoma ukiwa mbali”

Ameongeza kuwa nchi zipatazo 15 zimefunga shule kwa sehemu fulani na endapo hatua hizo zitatekelezwa katika ngazi ya kitaifa basi itawaacha wanafunzi wengine mamilioni bila kuhudhuria madarasa amesema Defourny na kuongeza kuwa “ni  muhimu na lazima kuchukulia maamuzi haya kwa kila hali ili yatekelezeke.” Pia amesema kwa mantiki hiyo “Ni muhimu kuendeleza uhusiano na wanafunzi, kuunda jamii na kuhakikisha wanajihisi ni sehemu ya hatua hizo na ni muhimu kwa wanafunzi, walimu na jamii. Na ndio maana ni muhimu kwa kila mkakati wa mwalimu kuchukuliwa na kuingizwa kwenye mtaala kutokana na mazingira ya sasa ya nchi husika. Na baada ya hapo mtaaala utatathiminiwa upya. Lakini tunasaidia kuhakikisha uhusiano huu wa elimu unaendelezwa ili kufundisha watoto wakiwa mbali kwa kila njia iwezekanayo.”

Mwendelezo

Kama sehemu ya hatua za kupunguza kusambaa kwa virusi vya Corona UNESCO inasaidia hatua zinazochukuliwa na nchi kupunguza athari katika mifumo ya elimu na kuwezesha masomo kuendelea hususani kwa wale wasiojiweza.

Mkutano kwa njia ya mtandao uliitishwa na shirika hilo na kuzihusisha nchi 73 ukishirikisha mawaziri wa elimu na manaibu mawaziri wa nchi zilizoathirika na zilizo na hofu ya mlipuko wa ugonjwa huo kwa lengo la kuhakikisha njia mbadala ya watoto kuendelea na masomo inapatikana.

Miongoni mwa mada zilizojadiliwa ni pamoja na kuzisaidia nchi katika maandalizi, kutumia suluhu jumuishi ya masomo ukiwa mbali, kubadilishana uzoefu, kutumia rasilimali za kidijitali ili kufungua fursa za masomo kwa wanafunzi wengi zaidi.

Shirika hilo linachagiza majukwaa ya elimu kusaidia muendelezo wa elimu bila kuathiri mtaala wa shule, kuwa na ushirikiano wa masomo kwa njia za mtandao na ufuatiliaji wa kimataifa wa shule na wanafunzi walioathirika na janga hili.

Fursa  na athari

UNESCO inasema kufunga shule hata kama ni kwa muda mfupi kunakuja na gharama kubwa za kijamii na kiuchumi. Na kubwa zaidi ni fursa ndogo sana za kuku ana kujiendeleza.

Na katika upande wa lishe shirika hilo linasema kufunga shule kunasababisha watoto wengi kukosa mlo ambao mara nyingi huupata shuleni. Lakini pia inasema wazazi walio na uwezo mdogo wa kuhakikisha watoto wao wanaweza kusoma wakiwa mbali wanaweza kukabiliwa na athari za kutokuwa na nyezo za kidijitali kuwezesha hilo.

Na mbali ya hayo UNESCO imeonya kwamba Watoto wengi wanaweza kuwa katika hatari ya kupata tabia mbaya kwa kuachwa nyumbani pekee yao.