Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Idadi ya waliokuwa na njaa 2018 ilipungua ingawa idadi ya nchi imeongezeka - ripoti

Mama na mtoto wake katika sehemu za Ethiopia ambako majanga ya asili kama vile ukame na mafuriko yanawasumbua tena ongeza mapigano kati ya makabila.
OCHA/Charlotte Cans
Mama na mtoto wake katika sehemu za Ethiopia ambako majanga ya asili kama vile ukame na mafuriko yanawasumbua tena ongeza mapigano kati ya makabila.

Idadi ya waliokuwa na njaa 2018 ilipungua ingawa idadi ya nchi imeongezeka - ripoti

Tabianchi na mazingira

Idadi ya watu waliokabiliwa na uhaba wa chakula mwaka 2018 ilipungua hadi kufikia milioni 113 ikilinganishwa na watu milioni 124 mwaka uliotangulia wa 2017.

Hiyo ni kwa mujibu wa ripoti ya kimataifa ya shirika la chakula na kilimo duniani, FAO, muungano wa Ulaya na shirika la mpango wa chakula duniani, WFP iliyotolewa leo mjini Brussels nchini Ubelgiji.

Hata hivyo ripoti hiyo imesema licha ya idadi hiyo kupungua idadi ya nchi zilizoathirika imeongezeka na kufikia 53 tofauti na 42 katika mwaka uliotangulia.

Kwa mujibu wa ripoti, takriban theluthi mbili ya watu wanaokabiliwa na njaa wako katika nchi nane tu ikiwemo Afghanistan, Jamhuri ya kidemokrasia ya Kongo, Ethiopia, Nigeria, Sudan Kusini, Sudan, Syria na Yemen. Katika nchi 17 njaa iliyokithiri ilisalia sawa au ilongezeka.

Mabadiliko ya tabianchi na majanga ya asili yalisukuma watu milioni 29 kukabiliwa na uhaba wa chakula mwaka 2018 na katika nchi 13 ikiwemo Jamhuri ya Kidemokrasia ya watu wa Korea na Venezuela hazipo kwenye tathmini kwa sababu ya ukosefu wa takwimu sahihi.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa ripoti, mkurugenzi mkuu wa FAO, José Graziano da Silva amesema licha ya kupungua kwa idadi ya watu wanaokabiliwa na njaa kali, idadi ya watu waliokabiliwa na njaa iliyokithiri bado ni kubwa na kwamba ni lazima kuongeza jitihada katika kujengea mnepo jamii zilizoathirika na zilizoko hatarini kwa ajili ya kuokoa maisha na mbinu za kujipatia kipato.

“Ili kutokomeza njaa, ni lazima tukabiliane na kiini chake ambavyo ni: mizozo, ukosefu wa usalama, ahtari za mbadiliko ya tabianchi”, amesema mkurugenzi mkuu wa WFP, David Beasley. 

Ameongeza kuwa, “wavulana na wasichana wanahitaji kulishwa vizuri na kuelimishwa, wanawake wanahitaji kuwezeshwa, miundombinu ya vijijini inapaswa kuimarishwa ili kuweza kufikia lengo la kutokomeza njaa.” Bwana Beasley ameongeza pia viongozi wa dunia wanahitaji kuchukua hatua na kusuluhisha mizozo sasa hivi.

Kwa upande wake kamishna wa muungano wa Ulaya kuhusu msaada wa kibindamu na usimamizi wa majanga, Christos Stylianides amesema ukosefu wa chakula unasalia kuwa changamoto kimataifa ambayo inahitaji juhudi za pamoja. Aidha Stylianides ameelezea juhudi za muungano wa Ulaya kuimarisha misaada ya kibinadamu.

Ripoti inalenga kuta wito wa kuimarisha ushirikiano ambao unalenfa kuzuia na kujiandaa katika kukabiliana na mahitaji ya dharura ya kibinadamu na mizizi yake ambayo inajumuisha pia mabadiliko ya tabianchi, misukosuko ya kiuchumi, mizozo na ufurushwaji. Halikadhalika inasisitiza umuhimu wa ushirikiano wa pamoja katika kukabiliana na maswala ya misaada na maendeleo ya mzozo wa chakula na kutoa wito kwa uwekezaji katika kuzuia mizozo na amani endelevu.