Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wataalam wa haki za binadamu watoa wito kwa mahakama  Misri kusitisha adhabu ya kifo

Jiji la Cairo Misri
Dominic Chavez/World Bank
Jiji la Cairo Misri

Wataalam wa haki za binadamu watoa wito kwa mahakama  Misri kusitisha adhabu ya kifo

Haki za binadamu

Wataalam wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa hii leo mjini Geneva Uswisi wamelaani kitendo cha kuteswa na kuuawa kwa wanaume tisa nchini Misri.

Kupitia taarifa iliyotolewa na ofisi ya  haki za binadamu hii leo, watalaam hao wamesema mamlaka za Misri zilitekeleza tukio hilo la kuwaua wanaume hao tisa alfajiri ya tarehe 20 mwezi huu wa Februari na kuwa tayari kulikuwa na rufaa na pingamizi katika mahakama kuu na pia kuwa walilazimishwa kwa njia ya mateso kukiri makosa.

Taarifa hiyo imewanukuu wakisema, "bado tuna wasiwasi zaidi kwamba kesi zingine kadhaa za watu waliohukumiwa zinasubiri mahakamani ,wakikabiliwa na  adhabu ya kifo , pia kuna ripoti ya ukosefu wa mchakato sahihi wa kisheria. Hukumu hizi zinaonekana kuwa hazizingatii moja kwa moja sheria na utaratibu wa Misri na kimataifa”

Mwezi Januari mwaka 2018, wataalam walitoa wito kwa  Misri kusitisha adhabu za kifo kufuatia ukiukwaji wa haki za binadamu wa mara kwa mara  na uonevu.

Ripoti ya haki za binadamu imebaini kwamba tangu kuanza kwa utawala wa  Rais el-Sisi mwezi Julai 2013, mahakama ya Misri imekazia hukumu 1,451 za vifo, kati ya rufaa ya kesi  2,443 zilizowasilishwa kutoka mahakama  za mwanzo.

Wataalam wameongeza kuwa adhabu  ya kifo nchini Misri inaweza kufanyika tu baada ya mchakato wa kisheria ambayo hutoa ulinzi kamili kwa mujibu wa  sheria ya kimataifa ya haki za binadamu, ili kuhakikisha haki inatendeka hadi hukumu ya mwisho.